Ndugu zangu Waandishi toka vyombo mbalimbali vya habari
nchini.
Asalam alaykum
Bwana Yesu asifiwe.
Nafurahi kukutana nanyi katika mkutano huu muhimu
nikiamini kuwa mara baada ya mazungumzo yetu, mtajitahidi kutumia weledi wa
taaluma yenu ili kutufikishia ujumbe wetu mbele ya jamii kwa madhumuni tulioyoyakusudia.
Tarehe 20 Agosti mwaka 2013 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti
wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed
Shein ametangaza na kufanya mabadiliko
katika Baraza lake la Mawaziri, kupangua Idara zilizokuwa zikisimamiwa na
Wizara mbalimbali na kuunda mpya nne visiwani Zanzibar.
Jumuiya ya UVCCM inampongeza kwa dhati hatua hiyo ya Rais Dk. Shein kwa mabadiliko hayo katika
Baraza lake la Mawaziri, UVCCM kwa kauli moja tunaahidi kushirikiana nae bega
kwa bega katika kuhakikisha majukumu yaliyokusudiwa yanatekelezwa hatua kwa
hatua.
Kitendo hicho cha Dk.
Shein licha ya kuhitaji kupongezwa na kuungwa mkono, kitaongeza shime, ari
na kasi ya utendaji na kuifanya Serikali
yake kuendelea na mipango pamoja na mikakati yake ya kutilia mkazo utekelezaji
wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2010/2015,
Dira ya Maenedeleo ya 2020 na Mpango wa Kupambana na Umasikini Zanzibar (MKUZA).
Katika kipindi cha miaka mitatu tokea aingie Madarakani,
Rais Dk Shein amekuwa kiongozi makini anayesimamia kwa vitendo na kufuatilia hatua
kwa hatua utendaji wa Serikali yake,
akiitisha vikao vya tathimini kila baada ya miezi mitatu maarufu kama “Bango
kitita “ kwa nia ya kujiridhisha, kudurusu na kusimamia majukumu ya kiserikali.
Mabadiliko alioyafanya ni ya msingi na maana yenye mashiko
na mantiki yakiwa na dhamira ya kuzidisha tija ya ufanisi wa majukumu ya
kiutendaji kwa manufaa na lengo la kuwatumikia wananchi kwa mwendo wa haraka na
usahihi.
UVCCM inachukua nafasi hii kusifu mabadiliko hayo muhimu pia
tukiwahimiza na kuwashauri Mawaziri,
Makatibu wakuu na Manaibu Makatibu wakuu waliobadilishwa toka Wizara moja hadi
nyingine kufanya kazi kwa bidii, juhudi, maarifa na uaminifu kwa nchi na watu
wake.
Dk Shein ni Rais Msikivu, Makini na Hodari wa kusoma alama
za nyakati na mabadiliko yake kwa lengo la kuwatumikia wananchi pia mwenye
ustaahamilivu wa kutosha katika uendeshaji wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar
iliyo chini ya mfumo wa Umoja wa Kitaifa.
Ahsanteni sana.
KIDUMU CHAMA
CHA MAPINDUZI
Shaka Hamdu Shaka
NAIBU KATIBU MKUU
UVCCM TANZANIA ZANZIBAR
0 Maoni