Unordered List


TAARIFA YA UMOJA WA VIJANA WA CHAMA CHA MAPINDUZI (UVCCM) KATIKA MAZUNGUMZO NA WAANDISHI WA HABARI WA VYOMBO MBALI MBALI KATIKA UKUMBI WA UMOJA WA VIJANA WA CCM MAKAO MAKUU DAR ES SALAAM JUMATANO 21 AUGUST 2013



Ndugu zangu Waandishi toka vyombo mbalimbali vya habari nchini.
Asalam alaykum
Bwana Yesu asifiwe.
Nafurahi kukutana nanyi katika mkutano huu muhimu nikiamini kuwa mara baada ya mazungumzo yetu, mtajitahidi kutumia weledi wa taaluma yenu ili kutufikishia ujumbe wetu mbele ya jamii kwa madhumuni tulioyoyakusudia.
Tarehe 20 Agosti mwaka 2013 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ametangaza na  kufanya mabadiliko katika Baraza lake la Mawaziri, kupangua Idara zilizokuwa zikisimamiwa na Wizara mbalimbali na kuunda mpya nne visiwani Zanzibar.
Jumuiya ya UVCCM inampongeza kwa dhati hatua hiyo ya  Rais Dk. Shein kwa mabadiliko hayo katika Baraza lake la Mawaziri, UVCCM kwa kauli moja tunaahidi kushirikiana nae bega kwa bega katika kuhakikisha majukumu yaliyokusudiwa yanatekelezwa hatua kwa hatua.
Kitendo hicho cha Dk. Shein licha ya kuhitaji kupongezwa na kuungwa mkono, kitaongeza shime, ari na kasi ya utendaji na  kuifanya Serikali yake kuendelea na mipango pamoja na mikakati yake ya kutilia mkazo utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2010/2015,  Dira ya Maenedeleo ya 2020 na Mpango wa Kupambana na Umasikini Zanzibar (MKUZA).
Katika kipindi cha miaka mitatu tokea aingie Madarakani, Rais Dk Shein amekuwa kiongozi makini anayesimamia kwa vitendo na kufuatilia hatua kwa hatua  utendaji wa Serikali yake, akiitisha vikao vya tathimini kila baada ya miezi mitatu maarufu kama “Bango kitita “ kwa nia ya kujiridhisha, kudurusu na kusimamia majukumu ya kiserikali.
Mabadiliko alioyafanya ni ya msingi na maana yenye mashiko na mantiki yakiwa na dhamira ya kuzidisha tija ya ufanisi wa majukumu ya kiutendaji kwa manufaa na lengo la kuwatumikia wananchi kwa mwendo wa haraka na usahihi.
UVCCM inachukua nafasi hii kusifu mabadiliko hayo muhimu pia tukiwahimiza  na kuwashauri Mawaziri, Makatibu wakuu na Manaibu Makatibu wakuu waliobadilishwa toka Wizara moja hadi nyingine kufanya kazi kwa bidii, juhudi, maarifa na uaminifu kwa nchi na watu wake.
Dk Shein ni Rais Msikivu, Makini na Hodari wa kusoma alama za nyakati na mabadiliko yake kwa lengo la kuwatumikia wananchi pia mwenye ustaahamilivu wa kutosha katika uendeshaji wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar iliyo chini ya mfumo wa Umoja wa Kitaifa.
Ahsanteni sana.
KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI

Shaka Hamdu Shaka
NAIBU KATIBU MKUU
UVCCM TANZANIA ZANZIBAR

Chapisha Maoni

0 Maoni