Unordered List


Tunaweza kujitoa Jumuiya ya Africa Mashariki (Tanzania)


Mh, Samweli Sitta
Rais wa Tanzania Jakaya Kikwete
Serikali ya Tanzania imesema inatafakari ushiriki wake ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na inaweza kujitoa ndani ya Jumuiya hiyo iwapo itaendelea kutengwa katika baadhi ya vikao.
Aidha imesema Tanzania haitambui vikao vinavyofanywa na nchi tatu zilizopo ndani ya Jumuiya hiyo ambazo zimekuwa zikizitenga Tanzania na Burundi.
Waziri anayehusika na masuala ya Afrika Mashariki wa Tanzania Samwel Sitta ameliambia Bunge la Tanzania kuwa makubaliano ya vikao hivyo vinavyofanywa na nchi za Kenya, Rwanda na Uganda yatatekelezwa na nchi hizo zinazofanya vikao hivyo kwa sababu vinafanyika nje ya utaratibu wa mkataba wa jumuiya hiyo.
Katika mikutano iliyofanyika hivi karibuni Tanzania na Burundi hazikualikwa kwenye vikao hivyo.
Kwa mujibu wa Waziri Sitta mikutano ya wakuu wa nchi za Rwanda, Kenya na Uganda ambayo ilianza kwa kuitenga Tanzania ilifanyika Entebbe nchini Uganda mwezi Juni mwaka huu na kufuatiwa na mkutano wa pili uliofanyika Agosti mwaka huu huko Mombasa nchini Kenya ambapo nchi hizo tatu bila kuishirikisha Tanzania walizungumzia uanzishaji wa himaya moja ya forodha.
Mambo mengine waliyozungumza wakuu hao ilikuwa uanzishaji wa visa moja ya utalii kwa nchi zao na matumizi ya vitambulisho vya uraia ambavyo vitatumika kama hati za kusafiria miongoni mwa nchi hizo.
Aidha Waziri Sitta amesema ndani ya mikutano hiyo pia walizungumzia kuanzisha mchakato wa kuanzisha shirikisho la nchi hizo.
Tayari Tanzania imeanza mazungumzo na nchi za Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo kuangalia ni kwa namna gani zitaanzisha ushirikiano nje ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kama zinavyofanya nchi za Rwanda, Uganda na Kenya.

Chapisha Maoni

0 Maoni