TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI.
Jumuiya ya Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) imepokea kwa
masikitiko makubwa taarifa ya kifo cha mjumbe wa tume ya mabadiliko ya
katiba Dr Sengondo Mvungi ambacho kimetokea katika hospitali ya Millpark
nchini Afrika kusini.
Uongozi wa UVCCM Taifa unatoa pole kwa
familia na ndugu wa marehemu, pia UVCCM inatoa pole kwa uongozi wa NCCR-
Mageuzi na kwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Jaji Warioba
pamoja na Vijana nchini kote ambao wamenufaika na Utaalamu na mafunzo.
Kama vijana tulihitaji sana mchango wa mawazo, hekima na utaalamu
kutoka kwake, hakika tumepoteza kiongozi shupavu, muadilifu na mzalendo
ambae ni mfano wa kuigwa kwa Vijana wa Taifa hili.
Kadhalika,
UVCCM inatoa pongezi za dhati kwa hotuba makini iliyojaa hekima, busara
na ushupavu wa Uongozi iliyotolewa na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi
na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Jakaya Mrisho
Kikwete.
Hakika vijana tumeridhishwa na maamuzi ya Mheshimiwa
Rais ya Kuendelea kuwa Mwanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC)
na tunapongeza maamuzi hayo yanayolenga kudumisha Umoja na Ushirikiano
wa Nchi za kiafrika katika kujiletea maendeleo.
Kwa kutambua
nafasi na manufaa yanayopatikana kwa vijana kutokana na fursa za
kiuchumi, kisiasa, kijamii, ajira nk UVCCM Inamuunga mkono Mheshimiwa
Rais kwa uamuzi wake huo.Pamoja na kuunga mkono uamuzi huo, UVCCM inatoa
angalizo kuwa ni vyema kwa nchi zote wanachama wa Jumuiya ya Afrika
Mashariki (EAC) kuendelea kuheshimu taratibu na kanuni za jumuiya hiyo
ili kuifanya endelevu, imara na mfano kwa nchi nyingine za Afrika na
Duniani kwa ujumla.
Ni lazima wazingatie kuwa Umoja na Mshikamano ndio nguzo ya maendeleo ya kweli ya Afrika.
Pia, Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) umesikitishwa na
tuhuma ambazo zimeripotiwa kwenye vyombo mbalimbali vya habari kutoka
kwa Mbunge wa Arusha Mjini (CHADEMA) Mheshimiwa Godbless Lema ambazo
amezielekeza kwa baadhi ya Viongozi wa Jumuiya akiwemo Mwenyekiti wa
Taifa wa UVCCM Ndugu Sadifah Juma kuwa amehusika na usambazaji wa Picha
chafu mitandaoni
Pamoja na kusikitishwa, UVCCM inazo taarifa
juu ya mgogoro unaoendelea katika Chama Cha Demokrasia na Maendeleo
(CHADEMA) na kwamba inamtaka Lema kutoelekeza tuhuma kwa UVCCM na
viongozi wake bali waangalie namna bora ya kushughulikia na kutatua
migogoro yao ya ndani ambayo imesababisha kuzushiana, kuchafuana na
kuvujishiana siri katika mitandao hasa ya kijamii.
UVCCM na
Viongozi wake inakana kwa namna yeyote ile kuhusika na usambazaji huo na
kwamba Jumuiya hii ni ya Vijana makini na wanaojitambua na inajielekeza
katika kufanikisha malengo ya kuundwa kwake ya kukisaidia Chama kushika
dola mwaka 2015.
Na kwamba UVCCM inalaani tabia ambayo
imeasisiwa na Vijana wa CHADEMA ya kukashifu, kuzomea na hata kutukana
Viongozi wa CCM na Serikali yake na kwamba yaliyomkuta Mhe Lema ni
matunda ya kazi waliyoiasisi wenyewe.
Imetolewa na: PAUL MAKONDAKATIBU WA IDARA YA HAMASA NA CHIPUKIZI UVCCM TAIFA
0 Maoni