Unordered List


KAMATI KUU YA CCM YAWAHOJI MAWAZIRI SABA





  Kamati Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), katika kikao chake kilichofanyika jana mjini Dodoma chini ya Mwenyekiti wake Rais Jakaya Kikwete imeibuka na masuala mazito kadhaa, ambayo leo, Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi Nape Nnauye (pichani) ameyaeleza wakati akizungumza na waandishi wa Habari, Katika Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Lumumba jijini Dar es Salaam.


Moja ya mambo ambayo Nape amezungumzia, ni kuhusu Kamati Kuu hiyo kuwahoji Mawaziri saba, kujibu kero au mambo kadhaa ambayo yaliibuliwa wakati wa ziara ya Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana iliyomalizika hivi karibuni katika mikoa ya Mtwara, Ruvuma, Mbeya na Njombe.

Nape  alisema, Kamati Kuu iliwahoji mmoja baada ya mwingine, kuanzia saa tano asubuhi hadi jioni, baada ya kila mmoja kufika akiwa ameandaa majibu ya tuhuma au hoja alizokuwa ametakiwa kujibu mbele ya Kamati Kuu hiyo.

"Kwa kuwa mawaziri hao tulikuwa tumeshawapelekea hoja zinazowahusu ambazo tulizipisha kwa kiranja wao Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, wengi wao walifika wakiwa na mafaili yenye majibu, ambapo waliingia na kujieleza mmoja baada ya mwingine, na baada ya maelezo ya kila mmoja wajumbe walitoa mapendekezo kwa Mwenyekiti, Rais Jakaya Kikwete", alisema Nape.

Hata hivyo Nape alisema, si vema kueleza kwenye vyombo vya habari kuhusu mapendekezo ambayo Kamati Kuu ilimshauri Mwenyekiti kuchukua, akisema kufanya hivyo itakuwa sawa na kumshinikiza kiongozi huyo kutekeleza mapendekezo yao kwa lazima na hivyo kuharibu maana nzima ya ushauri.

"Sisi tulichofanya ni kumpa mapendekezo, naye kwa mujibu na namna atakavyoona inafaa, atachukua hatua, ambavyo si lazima kumfukuza Waziri Kama wengi wanavyotaka iwe, bali anaweza kuchukua hatua yoyote ili mradi yeye mwenyewe kwa mamlaka aliyo nayo ataona ina manufaa yatakayotoa majibu ya kero zilizosaababisha kila mmoja wa mawaziri hao kuitwa mbele ya Kamati Kuu", alisema Nape.

IFUATAYO NI TAARIFA YOTE KAMA ALIVYOITOA NAPE LEO.
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM imekutana mjini Dodoma kwa kikao chake cha kawaida tarehe 13/12/2013. Kikao hicho kiliongozwa na Mwenyekiti wa Taifa wa CCM Ndg. Jakaya Mrisho Kikwete.

Pamoja na mambo mengine Kamati Kuu ilipokea taarifa ya ziara ya Katibu Mkuu wa CCM Ndg. Abdulrahman Kinana na baadhi ya wajumbe wa Sekretarieti kwenye baadhi ya mikoa nchini.
Kamati Kuu imepongeza ziara hizo kwa kuwa na mafanikio makubwa na kwa jinsi zilivyoongeza uhai wa Chama na zilivyojishughulisha na mambo na mahitaji ya wanachi.

Aidha Kamati Kuu imeipongeza sana Serikali kwa utekelezaji mzuri wa Ilani ya uchaguzi ya CCM kwenye maeneo yote ambayo Katibu Mkuu ametembea. Maeneo yaliyopongezwa ni pamoja na Miundombinu hasa barabara, hatua kubwa kwenye fursa na ubora wa elimu, maeneo ya afya na umeme vijijini.

Kamati Kuu iliwaita mawaziri saba kuja kutoa maelezo ya mambo mbalimbali yaliyoibuliwa kwenye ziara hizo za Katibu Mkuu wa CCM. Mawaziri hao ni;-

i). Ndg. Christopher Chiza- Waziri wa Kilimo,Chakula na Ushirika
ii). Ndg. Shukuru Kawambwa- Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi
iii). Ndg. Celina Kombani - Waziri wa Utumishi
iv). Ndg. Hawa Ghasia -Waziri wa TAMISEMI
v). Ndg. Abdallah Kigoda- Waziri wa Viwanda na Biashara
vi). Ndg. Mathayo David Mathayo- Waziri wa Mifugo na Uvuvi
vii). Ndg. Saada Mkuya- Naibu Waziri wa Fedha( kwa niaba ya Waziri wa Fedha).
Baada ya maelezo ya kutosha kutoka kwa mawaziri husika, Kamati Kuu iliagiza yafuatayo kwa Serikali;-

1.Kuhusu wakulima wa Pamba
(i). Serikali iangalie upya upatikanaji wa pembejeo za ruzuku kwa wakulima wa Pamba nchini.
(ii). Uwepo wa mbegu bora ni muhimu lakini ni vizuri pakawa na ushindani unaozingatia ubora ili kuondoa ukiritimba wa mtengenezaji mmoja, hivyo kusaidia bei kuwa nzuri kwa wakulima. Hata hivyo Chama kimeiagiza serikali kutowalazimisha wakulima kutumia mbegu ya Quiton badala yake elimu itumike zaidi badala ya nguvu. Serikali imetakiwa kuangalia upya utaratibu wa kutoza bei ya mbegu ya Quiton kwa dola za kimarekani badala ya pesa ya kitanzania,wakizingatia mbegu hiyo inazalishwa nchini.
(iii).Kamati Kuu imepongeza juhudi za Serikali kuvutia wawekezaji kwenye viwanda vya pamba mjini Shinyanga, hata hivyo imeitaka Serikali kuangalia upya urasimu katika uwekezaji wa viwanda nchini hasa vinavyoongeza thamani ya mazao na kutoa ajira nyingi nchini.

(iv). Kuhusu kilimo cha mkataba kwa wakulima wa Pamba, Serikali imetakiwa kuratibu utaratibu wa kilimo hicho cha mkataba ili kuhakikisha kunakuwa na sheria na kanuni zinazosimamia mfumo huo, ili kuwe na haki kwa pande zote mbili. Aidha wakulima wasilazimishwe kufanya kilimo cha mkataba bali waingie kwa hiari yao wenyewe.

2. Kuhusu wakulima wa Korosho.
(i). Pamoja na kuridhishwa na hatua za muda mfupi kwa msimu wa korosho kwa mwaka 2013/2014 ambazo zimesaidia bei na soko kuwa afadhali, bado Kamati Kuu imesisitiza Serikali kujipanga kutatua tatizo la korosho kwa suluhisho la kudumu kwa kuhakikisha korosho ina banguliwa nchini.

(ii). Serikali imetakiwa kuangalia upya orodha ndefu ya makato wanayokatwa wakulima hasa wa korosho na vyama vya msingi au mamlaka zinginezo ili kuondoa makato yasiyo ya lazima ili kuongeza kipato cha mkulima.

(iii). Serikali pia imetakiwa kuangalia upya mfumo wa uendeshaji wa vyama vya ushirika nchini ili uwe ni ule wenye tija kwa wakulima na nchi kwa ujumla badala ya huu wa sasa unaotoa mwanya kwa walaji kujipenyeza.

3. Kuhusu pembejeo za ruzuku
(i). Kamati Kuu imepokea taarifa ya malalamiko ya wakulima juu ya ufanyaji kazi wa mbolea ya Minjingu na kuagiza kuwa pamoja na kuendelea na utafiti wa nini kinachotokea kwenye mbolea hiyo ya Minjingu kiasi cha kuleta malalamiko yote hayo, wananchi wawe huru kutumia mbolea wanayoitaka badala ya kulazimishwa kutumia mbolea wanayoilalamikia ya Minjingu.

(ii). Serikali iangalie utaratibu bora wa kuratibu swala zima la pembejeo za ruzuku ili lifaidishe zaidi wakulima walio wengi badala ya utaratibu wa sasa ambao licha ya kulalamikiwa na wakulima unaotoa mwanya kwa watu wachache kutumia vibaya utaratibu huo kuiibia serikali na wakulima.

4. Kuhusu wakulima wa mahindi.
(i). Pamoja na Serikali kuanza kulipa madai ya wakulima wa mahindi kwa mikoa ya Ruvuma baada ya ziara ya Katibu Mkuu kwenye maeneo hayo, bado serikali imetakiwa kumalizia malipo yaliyobaki na kuhakikisha wanakomesha utaratibu wa kuwakopa wananchi mazao yao bila kuwalipa.

(ii). Utaratibu uwekwe wa kufanya tathimini mapema ya mahitaji na uwezo wa kununua  mahindi wa Serikali ili kuepusha utaratibu wa kuchukua mahindi ya wakulima bila kuwalipa.

5. Kuhusu madai mbalimbali ya waalimu.
(i). Kamati Kuu imesisitiza kupandishwa vyeo na kulipwa stahiki  zao waalimu ni haki yao ya msingi hivyo lazima itekelezwe bila kuwa na visingizio na ifanyike kwa haki.

(ii). Kamati Kuu imeiagiza Serikali kukamilisha haraka uhakiki wa madai ya waalimu na kuwalipa haki zao zote mapema iwezekanavyo. Lakini Kamati Kuu imeitaka Serikali kuhakikisha madeni haya hayazaliwi tena kwa kuweka mfumo utakao zuia madeni haya kuzaliwa.

(iii). Kuhusu wakuu wa idara mbalimbali wasiotenda haki kwa waalimu, na wale wanaotumia lugha mbaya na za kejeli kwa waalimu wakibainika wachukuliwe hatua mara moja.

(iv). Pamoja na kuwa Serikali inaangalia utaratibu bora wa kuboresha mawasiliano kati ya wizara zinazohusika na kusimamia waalimu, Kamati Kuu imeitaka Serikali jambo hili lifanyike mapema ili kupunguza malalamiko ya waalimu.

6. Kuhusu ubadhirifu kwenye Halmashauri.
(i). Kamati Kuu imekemea watendaji wachache wanaojihusisha na ubadhirifu kwenye Halmashauri mbalimbali nchini. Imewataka madiwani wa CCM kuwa wakali na wasiamamie vizuri halmashauri zao kuhakikisha fedha inatumika kwa malengo yaliyokusudiwa na kupata thamani ya fedha.
(ii). Aidha Serikali imetakiwa kuchukua hatua kali na kwa haraka kwa wote wanaobainika kufanya ubadhirifu, ili iwe fundisho kwa wengine.

(iii). Serikali imeshauriwa kuangalia upya sheria kama zinakidhi mahitaji ya wakati na mazingira ya sasa ili kuongeza uwezo wa udhibiti na kuokoa pesa za walipakodi zinazopotea kwa walafi wachache kwenye Halmashauri mbalimbali nchini.

7. Kuhusu tatizo la Maji nchini.
Kamati Kuu ilipokea taarifa ya tatizo kubwa la maji nchini, ambalo lilijitokeza kila sehemu aliyotembelea Katibu Mkuu. Chama kimeishauri Serikali kuchukua juhudi na mkakati wa makusudi na dharura kulitafutia ufumbuzi wa haraka na wakudumu tatizo la upatikanaji wa maji nchini.

8. Kuhusu migogoro ya Aridhi, Wafugaji na Wakulima.
Pamoja na kupokea taarifa juu ya migogoro mbalimbali ya wakulima ,wafugaji na wakulima nchini, kamati kuu imepongeza uamuzi wa bunge kuunda Kamati teule ya bunge na uamuzi wa kuiagiza kamati ya kudumu ya bunge ya aridhi, maliasili na mazingira kuchunguza migogoro hii na kutoa mapendekezo juu ya namna bora ya kuimaliza kabisa migogoro hii.

Aidha kamati kuu imeitaka Serikali na wabunge wa CCM kuzijadili kwa makini ripoti hizo na kufikia hitimisho la migogoro hii nchini. Hata hivyo Kamati Kuu imeitaka Serikali kuangalia upya utaratibu uliotumika kuwamilikisha watu wachache maeneo makubwa ya aridhi, ambao wameshindwa kuyaendeleza badala yake wanayatumia kuwakodishia wakulima wadogo.

Aidha maagizo yote haya yatatolewa taarifa kwenye Chama mara kwa mara, ili kuwezesha Chama kufuatilia utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2010/2015.

Imetolewa na;-
Nape Moses Nnauye
Katibu wa Itikadi na Uenezi
14/12/2013

Chapisha Maoni

0 Maoni