Unordered List


MP. Dkt, Hamisi Kigwangalla na PESA ZA USHURU WA HUDUMA kutoka Resolute Tanzania: (Nzega)

PESA ZA USHURU WA HUDUMA kutoka Resolute Tanzania:
Mbunge huyu Kijana wa Jimbo la Nzega na Mwenyekiti wa TAMISEMI  Alianza kwa Kusema hivi

 "Ndg. Gisberth Kabamba na ndugu zangu wengine wote mnaonisoma hapa. Kuna maneno mengi sana yanayosemwa kuhusiana na upatikanaji wa pesa za ushuru wa huduma kutokana na uwepo wa mgodi wa uchimbaji dhahabu Lusu Nzega. Kuwa ni nani haswa aliyezileta pesa hizo? Japokuwa si muhimu sana kumjua aliyezileta bali kushukuru kwamba tu kuwa zimekuja. Kwa faida ya historia na kuweka sawa kumbukumbu ni vizuri hili jambo likaelezwa.
Acha leo niseme na mimi mnisikie. Siku zote niliona si muhimu sana kuzungumzia hilo maana niliamini ukweli unajulikana. Na kwa tabia ya ukweli, kuwa haubadilishwi na uongo, niliamini ukweli utabaki kuwa ukweli na hivyo sikuona haja ya kueleza. Pia niliamini kuwa wananzega wenzangu wanajua ni nini kilifanyika mpaka pesa zile zikapatikana. Na nilijua watu makini wakifanya tafakuri tunduizi hawatopata tabu kujua kuwa mgodi huu ulikuwepo Nzega kwa zaidi ya miaka 14, na kulipita wabunge na madiwani wengi na walijua kuna sheria ya kudai ushuru wa huduma, sasa nini kiliwafanya wao hawakufanikiwa kuzidai pesa hizi na leo zimefanikiwa kudaiwa. Kuna kitu gani tofauti hapo kimetokea?
Hadithi ya kufikia pesa hizi kupatikana ni ndefu na mimi binafsi sikupenda kuyasema mengine ambayo hayakupaswa kusemwa kwenye umma.
Kwanza, historia ya jambo hili ikoje? Wakati nagombea na hata baada ya kuchaguliwa kuwa MB wa Nzega, nimejikuta na tabia ya kutembelea sehemu mbalimbali za kijamii ambazo zinanipa heshima ya kuhojiwa maswali na kuyajibu. Utamaduni huu niliukuta kwa mara ya kwanza sana sana pale kwenye kijiwe maarufu cha BBC, ambacho wengi husema kina wapinzani wengi wanaofika pale kujadili siasa za Nzega, Kitaifa na Kimataifa. Pale nilikutana na wazee ambao walinifikishia malalamiko yao ya madai kule Lusu na malalamiko yanayohusiana na mgodi wa Golden Pride. Nikiwa kwenye kampeni kama mgombea wa CCM, kuna watu wa maeneo ya mgodi walikataa kupigia kura CCM kwa kuwa waliahidiwa na mgombea wa CHADEMA kuwa akishinda atahakikisha wanalipwa stahiki zao. Nikaenda binafsi kuongea nao, bahati nzuri nikakuta wakiwemo watu wangu kama akina Mzee Jailos, Mzee Sudi (Mungu amrehemu) na akina Bilantanye, nikawasihi wasinisuse wanisaidie tuchukue Ubunge nami nitawapigania kufa na kupona.
Niliposhinda Ubunge niliamua kuanza na jambo hili. Nikifanya mikutano ya kushukuru wananchi kwa kunichagua nilifanya mkutano viwanja vya parking na watu wale walinisomea risala huku wakitoa machozi, niliumia sana, nikasema nitapigana pembeni yao. Nikaanza utafiti wa namna gani nifanye ili niweze kuwasaidia. Niliandika barua nyingi ambazo hazikuzaa matunda. Nilipigana mpaka kuhakikisha hili jambo limemfikia Mhe. Waziri Mkuu na mwishowe kwa Mhe. Rais, kwa namna na sura tofauti tofauti. Nimewasilisha hoja binafsi kuhusu jambo hili zaidi ya mara 10 bila mafanikio. Nimechangia Bungeni zaidi ya mara 5, maswali zaidi ya mara 3 bila mafanikio. Nimefanya mikutano na mawaziri kuanzia Ngeleja mpaka Prof. Muhongo bila mafanikio. Kutokufanikiwa kwangu hakukunifanya nichoke ama niache kufuatilia. Nilikomaa zaidi na kubuni mbinu mpya kila siku. Sikukata tamaa. Niliendelea kupigana. Wasionipenda walinipa majina mengi, wengine wakithubutu hata kupeleka fitna na majungu kwa wakubwa kwenye chama change eti mimi ni mpinzania!
Mara kwa mara nilikutana na wale wachimbaji nikiwapa mrejesho wa ninachokifanya. Na wao walinipa moyo kwa kuendelea kuniamini na kuvumilia bila kuchoka.
Nikaamua kutumia hatua kali zaidi za nguvu ya umma - tukaomba kibali cha kuandamana, tukanyimwa, tukafanya mikutano haramu tukapata matatizo. Mwishowe Mkuu wa Mkoa akaamua kutupa kibali tuandamane kuonesha hasira zetu. Nikatoa hotuba kali sana pale Mwabangu huku nikijiapiza kwenda kuvamia mgodi kama wazungu hawatokubali kulipa pesa zote tunazodai. Maafisa uhusiano wa mgodi walikuwepo.
Niliendelea kupigana kutokea kila kona. Katika Baraza la madiwani, niliamua kuliingiza jambo hili kama hoja yangu binafsi nikimtaka DED wa Nzega, enzi hizo Ndg. Kyuza Kitundu, awaandikie ‘demand note’ watu wa mgodi ili wasipolipa twende tukakamate mali zao zenye thamani ya deni hili, kwa mujibu wa sheria na sheria ndogo (by-laws) zetu, akabisha sana kwa woga wa kuanzisha mapambano na shirika hili kubwa la kimataifa, niliendelea kumbana kwenye vikao mpaka kufikia kutishia kumwajibisha kwa mujibu wa kanuni kwa kutotekeleza maamuzi ya vikao – akaamua kuandika! Nao wakaanza vita ya kisheria kwa kutujibu kisheria kupitia mawakili wao, REX Attorneys. Vita hii haikuzaa matunda baada ya kukwamishwa na mazungumzo yaliyoanzishwa na Mkuu wa Mkoa. Sikuchoka. Niliendelea kufuatilia.
Ni siku tulipoandamana, wakaona umati ulioshiriki na ukali wa hotuba na michango yetu kwenye mkutano ule wa Mwabangu na wakizingatia tishio la kuvamia mgodi ndani ya siku tisini ndipo nikapigiwa simu na Waziri Muhongo akinitaka tuonane Dodoma tuzungumze kuhusu jambo hili wakiwepo wawakilishi wa mgodi na wawakilishi wa Halmashauri ya Nzega. Na kwenye mazungumzo yangu na Muhongo ambaye alimuita Naibu Waziri Madini Massele ndipo wakaniambia tuzungumze kwanza kabla ya kuchukua hatua hizo kali, nilimuelewa na nikakubali. Katika mkutano huu nilioneshwa email zilizotoka kwa watu wa Resolute wakilia lia kuwa MB wa Nzega Dkt. Hamisi Kigwangalla ni mkali sana na ana nia ya kuchafua hali ya hewa pale mgodini na kwamba wanahofia usalama wao na ule wa mali zao.
Baada ya miadi hii ya kukutana tulifunga safari ya madiwani na watumishi wa Halmashauri kuambatana nasi Wabunge wawili Dodoma kuhudhuria kikao hiki. Kikao hiki na hoja zote za madai haya zilitolewa na mimi maana nilikuwa na uelewa mpana zaidi wa suala hili kutokana na ufuatiliaji wangu wa kina na wa muda mrefu. Baadhi ya madiwani waliokuwepo ni mashahidi kwenye hili. Wahe. Patrick Gululi Mbozu, Pele Izengo Anthony, Bazilio Furaha Lazaro, Sawaka Paraxedes Shita na Kalori Ng’hwagi Masanja walikuwepo, waulizeni watawaambia ukweli kama mkitaka kuthibitisha hili. Mhe. Selemani Zedi (MB) alikuwa na dharura ya kikazi na hivyo alikaa mwanzoni tu wakati wa utambulisho kisha akaomba udhuru akatoka. Kuna saa niligonga hadi meza kwa hasira mpaka wakawa wananituliza. Kwa hoja niliwasambaratisha wazungu na kuhakikisha Naibu Waziri Massele na wataalamu wake wanakaa upande wa kuamua kwa faida ya Nzega.
Mhe. Selemani Zedi alinisaidia sana kuhakikisha tunapata mkataba kamili baina ya Resolute na Serikali ya Tanzania, kipindi hicho akiwa mjumbe wa Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini. Kabla sijaupata mkataba huu, nilipewa kurasa zote nyeti za mkataba na rafiki zangu watumishi wa umma na ndizo zilizonitia nguvu ya kuendeleza mapambano tangu awali bila wasiwasi wa ‘kuchemka’ ama kushindwa.
Mkuu wa Wilaya ya Nzega, aliyeondoka, Mama Florence Horombe, mumkumbuke wana Nzega zaidi kwa kuniweka ‘lupango’ bila sababu za msingi, na kwa kunizuia nisiingie kwenye geti la mgodi kwenye kikao cha kujadiliana kuhusu madai haya. Kama si Mhe. Zedi naye kukataa kuingia na madiwani, watumishi wote wa ofisi ya DED na ya Mkuu wa wilaya kumfuata, mimi nikiwa kimya tu, wakisema 'kama aliyeanzisha hoja hii hatakiwi humo ndani, naye ndiye analijua jambo hili, sisi sasa tutaingia kusema nini?’ ‘…basi nasi hatuingii, tugeuze magari turudi Nzega mjini'. Msimamo huu ulikuwa muhimu kwa ‘movement’ nzima maana ilionesha kuwa si ‘wehu’ wangu tu unaosababisha mvutano huu na kwamba ni mtazamo wa watu wengi ‘wazima’ na kwamba tuna msimamo wa pamoja kwenye jambo hili kama wilaya.
Mumkumbuke pia Katibu wa CCM wilaya Nzega wakati huo Ndg. Kajoro Vyohoroka kwa kuandika barua kwa viongozi na wanachama wenzangu wote wa CCM akiwaamrisha wasishiriki maandamano ya Mbunge kudai haki za Nzega; na pia kwa kuandika barua kwa OCD Nzega kumtaka asitishe maandamano hayo kwa kuwa CCM haijabariki (kumbe ni yeye binafsi tu hajabariki maana hata mimi ni CCM na hakukuwa na kikao kilichotoa msimamo huo).
Pia mnapofuatilia jambo hili, msimsahau Katibu wa CCM Mkoa wa Tabora Ndg. Iddi Ali Ame kwa kuamua KUYARUHUSU maandamano hayo kwa kuwa aliona yana maslahi ya umma ninaouwakilisha.
Pia msiusahau mchango wa Mwenyekiti wa Halmashauri na Mkurugenzi wake na zaidi mwana Sheria (mke wa Ndg. Mwaluko) aliyetushauri vizuri kwenye vikao na kusema Mbunge Dkt. Hamisi Kigwangalla ana hoja nzito iliyosimama kisheria. Na kwa kuendelea kunishauri mara kwa mara na kunipa taarifa za namna alivyoendelea kujibishana nao kwa barua.
Huu ndiyo mchango wa kila mtu (kwa ufupi tu). Sitaki kuwa mtoa hukumu kuwa ni nani alizileta pesa zile. Niwaache mtoe hukumu wenyewe. Kuna watu walinikejeli kwa kuandika waraka wa kunikashifu kwenye mitandao wakidai kuwa sintofanikiwa kwenye madai hayo lakini pesa zilipotoka walikuwa wa kwanza kudai zimeletwa na watu wanaowajua wao na wakitoa maelekezo ya namna ya kuzitumia pesa hizo. Mpaka leo pesa hizi hazijatumika kwa sababu ya mivutano na chokochoko inayofanywa na wanasiasa uchwara (ambao mwanzoni walidharau harakati hizi). Nimeyazoea haya kwa kuwa ni siasa ndogo ndogo, na kwa mwanamabadiliko na mwanamapinguzi kama mimi sipati tabu hata kidogo, ila najituma kufanya kazi zangu kwa bidii na weledi wa hali ya juu nikijua ipo siku wananzega watanikumbuka. Kama siyo mnaoishi leo, basi watakaokuja kuishi baadaye."

Alimaliza hivo alipokuwa akiongea na wana Nzega 

Chapisha Maoni

0 Maoni