Unordered List


MANGULA ATUA RASMI KALENGA KWA KISHINDO

*Asema Chadema wanalia kilio cha mamba
*Ni kwa kukimbiwa kutokana na kudhuru watu.
*Asema hatapanda jukwaani, ataratibu tu kampeni
*Asisitiza anayegombea Kalenga si Mgimwa ni CCM

NA BASHIR NKOROMO, IRINGA
MRATIBU wa Kampeni za CCM katika uchaguzi mdogo jimbo la Kalenga, Iringa Vijijini, Makamu Mwenyekiti wa CCM (Bara), Philip Mangula amesema, madai ya Chadema kwamba CCM imepeleka mamluki katika jimbo hilo ni kilio cha mamba, baada ya chama hicho kukimbiwa kutokana na vitendo vyake vya kudhuru watu ikiwemo kuwatoboa macho kwa bisibisi na kuwamwagia tindikali.

Hivi karibuni Chadema wanadaiwa kumtoboa jicho kwa bisibisi Alphonce John wakati wa kampeni za uchaguzi mdogo wa udiwani mjini Kahama, na pia wanadaiwa kumpa ulemavu wa kudumu kwenye sura Mussa Tesha baada ya kumwagia Tindikali wakati wa uchaguzi mdogo uliofanyika Igunga 2012.

Mangula amesema mbali na vitendo vya kutoboa macho na kumwagia watu tindikali, ambavyo Chadema inadaiwa kufanya, pia chama hicho kimeogofya wananchi kwenda kwenye mikutano yake, kutokana na kujiwekea histoa mbaya ya watu kuuawa katika mikutano yake kadhaa ambapo sasa wamefikia watu zaidi ya wanane tangu chama hicho kuanzishwa.

Makamu Mwenyekiti huyo wa CCM Bara, ametoa ufafanuzi huo baada ya mwandishi mmoja wa habari kutaka kujua CCM ilikuwa na maoni gani kuhusu tuhuma ambazo zimetolewa na Chadema, kwenye mkutano wake na waandishi, leo, Machi 3, 2013 ikisema kwamba CCM imeingiza watatu iliowaita majambazi, kutoka mikoani kwa nia ya kufanya fujo jimboni Kalenga nyakati za kampeni.

Mangula ambaye amewasili mjini Iringa, leo, Machi 3, 2013, akiwa tayari kuingia katika jimbo la Kalenga, ambako alisema atapiga kambi hadi Machi 16, mwaka huu uchaguzi ukapofanyika na CCM kuibuka Kidededea, alisema, CCM haina sababu ya kuingiza waovu jimboni kwa kuwa siyo jadi yake na inatambua thamani ya amani kuwepo katika eneo lolote.

"CCM inatambua umuhimu wa amani mahala popote, na kwa bahati nzuri mimi binafsi ninao uzoefu na mifano mingi kuhusu madhara ya kutoweka amani hivyo kama kiongozi na mratibu wa kampeni za CCM katika jimbo hili la Kalenga siwezi kuruhusu CCM kufanya mambo ya kijinga kiasi hicho", alisema Mangula na kuongeza;

"Wakati Chadema wanajaribu kujikosha kwa wananchi kwa kulia machozi ya mamba, sisi tumeshajua kwamba chama hicho kimeingiza mamluki kumi kutoka nje ya Iringa ikiwemo Tarime na Temeke, na kuwatawanya katika kata mbalimbali. Na hili sisi tunalisema kwa ushahidi wa kutosha, tunawajua mamluki hao na hata majina yao tunayo..tunasubiri kuchukua hatua za kisheria kabla ya kuwataja".

Katika hatua nyingine, Mangula alilaani hatua ya Chadema kutumia ufukara wa mtoto mmoja na familia yake, kuombea kura kwa wananchi katika kampeni zake zinazoendelea za kumnadi mgombea wa chama hicho katika jimbo la Kalenga, akisema kwamba hatua hiyo, mbali na kwamba siyo sahihi katika siasa lakini ni kumdhalilisha mtoto huyo umasikini wake.


"Hawa Chadema hawana utu kabisa, inawezekanaje Meneja wa kampeni wa chama hicho anambeba mtoto wa mtu na kumnadi kwa wananchi kwamba amevaa sare chakavu za shule na kwamba ni kiongozi wa CCM. Hili jambo limetusikitisha sana kwa sababu ni kuivunjia heshima CCM na pia kumdhalililisha mtoto huyu kwa umasikini wake", alisema Mangula alionyesha picha iliyochapishwa kwenye gazeti la Tanzania Daima, Meneja wa kampeni za Chadema akiwa amembeba mtoto aliyevaa nguo chakavu za shule.

Mangula aliwataka wana-CCM katika jimbo la Kalenga kutokuwa na hofu yoyote, wakati wa kampeni na siku ya kupiga kura kwa sababu anaamini ulinzi wa serikali upo wa kutosha.

Akizungumza na baadhi ya viongozi wa CCM mkoa wa Iringa, Mangula aliwataka kutumia muda wa kampeni kuwajulisha wana-CCM na wananchi kwa jumla kwamba wanayemnadi kushinga ubunge si Godfrey Mgimwa, bali ni CCM ndiyo inayowania kiti hicho.

Chapisha Maoni

0 Maoni