Unordered List


CHADEMA YAMTELEKEZA MGOMBEA WAO CHALINZE


Katibu wa NEC Itikadi na Uenezi akisisitiza jambo wakati wa mkutano wake na Waandishi wa Habari uliofanyika leo Chalinze.
 Katibu wa NEC Itikadi na Uenezi Nape Nnauye akizungumza na waandishi wa habari Chalinze, ambapo pamoja na kuwaambia tathmini ya CCM lakini aliwaambia kuhusu namna ambavyo vyama vingine havijakuwa kidemokrasia kiasi cha kuanza kubaguana hadi kwenye kampeni.

Mgombea wa CHADEMA Mathayo Torongey anayedaiwa kutelekezwa.


  •          Wabunge wagoma kuchangia kampeni Chalinze
  •          Washindwa kupeleka helkopta Chalinze
  •        Yadaiwa kisa ni ubaguzi walionao


Na Mwandishi Wetu,Chalinze

Torengei ametelekezwa na Chadema kwasababu ya kabila lake na ukanda wake na ndio maana hata helkopta wameshindwa kuipeleka ili kumsaidia kwenye kampeni.
Hayo yalisemwa jana na Katibu na Itikadi na Uenezi wa CCM Nape Nnauye wakati akitoa tathimini ya hali ya kampeni za uchaguzi jimbo la Chalinze.
Alisema kuwa viongozi wa Chadema wameonesha wazi kuwa hawana nia ya kumsaidia Torengei na sababu kubwa ni moja tu kuwa si mwenzao.
" Wabunge wa Chadema wamekuwa na utamaduni wa kuchanga fedha zinapotokea chaguzi lakini kwa huyu mgombea wao wa Chalinze wamegoma kufanya hivyo.
"Wamekuwa wakifanya ubaguzi lakini sasa ni dhahiri kuwa wameonesha kile ambacho kipo moyoni mwao.
"Ukifanya uchunguzi utabaini hakuna mahali ambapo Chadema hawakutumia helkopta katika uchaguzi mdogo ambapo walishawahi kutumia helikopta kwa uchaguzi wa Udiwani tu Arusha.
Alifafanua kuwa Torongei ametapeliwa na Chadema na hilo litakuwa fundisho kubwa kwake na kwamba ameingizwa mkenge.
"Anachotakiwa kujua jamaa hao ni matapeli na ameingizwa mkenge.Tunajua baada ya uchaguzi huu si atashindwa kupata kura bali atakuwa amefilisika,"alisema Nape.
Aliongeza kutokana na kumsusia uchaguzi huo, hata vijana ambao wameletwa na Chadema kwa ajili ya kufanya vurugu wanaishi maisha ya kuomba omba.
"Wamewaleta vijana lakini nao wanaishi maisha ya kubahatisha.Wamefikia mahali vijana wao wanakuja kuomba fedha ya kula tunawapa.
"Hivyo kama wao nao wameishiwa wasione aibu maana kitendo cha kumsusa mgombea wao, wachache waliopo wanaishi maisha magumu sana,"alisema Nape.
Akizungumzia ushindi wa chama hicho, Nape alisema kwa hali ilivyo watashinda kwa zaidi ya asilimia 94.
"Ushindi wetu katika uchaguzi unaotarajia kufanyika Aprili 6 ambayo itakuwa Jumapili ni zaidi ya asilimia hizo.Wapinzani hawana lolote na watashindwa vibaya kuliko wanavyotarajia,"alisema.
Kuhusu kampeni zinazoendelea, alisema zinakwenda vizuri lakini wapinzani hasa Chadema wanafanya hujma za kuiba shahada za kupigia kura kupitia watoto ambao wanawapa fedha ili waziibe kwa wazazi.
"Tunazo taarifa kuwa kuna baadhi ya maeneo wananchi wanalalamika Chadema wanatumia watoto kuiba shahada hizo kwa lengo la kupunguza ushindi wa CCM pia kutoa taarifa za uwongo kuhusu tarehe ya kupiga kura kwa kuwaaminisha wapiga kura kuwa uchaguzi utakuwa mwezi wa sita tarehe 6,"alisema Nape.

Chapisha Maoni

0 Maoni