Unordered List


DK. ASHA-ROSE: HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA WA SHERIA NI MUHIMU KWA MAENDELEO


 Na Mwandishi Maalum,   New  York
Waziri wa  Sheria na  Masuala ya Katiba, Dk. Asha-Rose Migiro( Mb) amesema, ajenda za maendeleo endelevu baada ya 2015 zijielekeze zaidi katika kuyawezesha makundi ya jamii yaliyo katika mazingira magumu.
Ameyasema hayo  siku ya jumanne,wakati alipokuwa akichangia hoja kuhusu  mchango wa  haki za binadamu na  utawala wa sheria katika kuunga mkono juhudi za kitaifa na kimataifa kuelekea  upunguzaji wa umaskini na maendeleo endelevu.
Waziri Migiro alikuwa mmoja wa wanajopo wanne waliojadili hoja hiyo iliyoanzishwa na Naibu  Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa,  Bw. Jan Eliasson ikiwa ni sehemu ya  mkutano wa siku mbili  ulioandaliwa na  Rais wa Baraza  Kuu la Umoja wa Mataifa na kuwashirikisha wawakilishi kutoka  mataifa mbalimbali.
Pamoja na  kusisitiza  haja na umuhimu wa  ajenda mpya  za maendeleo kujielekeza katika  kuyawezesha makundi hayo ya jamii. Waziri Migiro ameongeza pia kwamba   ni muhimu jumuiya ya kimataifa ikajikita  pia katika kupunguza  pengo la uwiano wa maendeleo kati ya maeneo ya mijini na vijijini.
“ Ni  muhimu kwamba kila sehemu ya jamii ikawezeshwa ili iwe na fursa ya kupata haki,  haki  ya kumiliki mali,  ikiwamo haki  ya  kumiliki na  kurithi ardhi na haki za ajira zenye  ujira sawa kwa kazi sawa” akaeleza Migiro na  kuongeza.
Akasema ili hayo na mengineyo yaweze kutekelezwa ni  vema basi  suala la haki za binadamu na utawala wa sheria  vikawa sehemu muhimu ya Ajenda za Maendeleo baada ya 2015 na  vilevile kwa  Malengo  Endelevu ya Maendeleo.
Akizungumza  kuhusu  utekelezaji wa  Malengo ya Maendeleo ya  Millenia ( MDGs),  utekelezaji wake unaelekea ukingoni.Waziri wa Sheria na Masuala ya Katiba, anasema. Tangu kupitishwa kwa malengo hayo mwaka 2000  nchi nyingi hasa zile zilizokuwa zikikabiliwa na changamoto nyingi za maendeleo  zilijiweka sera na  vipaumbele  katika utekelezaji wa malengo hayo.
“   Tumeshuhudia  nguvu za pamoja katika ngazi ya kitaifa na ya kimataifa katika kuhakikisha kwamba MDGs inakuwa  kiungo cha    ajenda za maendeleo”.  Na  kuongeza kwamba pamoja na  mafanikio  ya kuridhisha katika utekelezaji wa  MDGs hizo, bado  kuna mengi yakutekelezwa”. akasisitiza  Waziri.
Akizungumzi nafasi ya Tanzania katika utekelezaji wa MDGs,  Waziri amesema,  Tanzania imefanikiwa katika utekelezaji wa malengo mengi, ingawa changamoto  kubwa  imebaki katika kulitafutia ufumbuzi pengo   lililopo kati ya  miji na vijiji ili kuhakikisha kwamba watu wote wanakuwa na fursa na haki sawa ya kunufaika  na maendeleo endelevu.
Akasema  anauhakika kwamba  nchi nyingi zinakabilia na changamoto hiyo ya  utofauti mkubwa wa kimaendeleo kati ya  maeneo ya mijini na vijijini.
“Pengo kati ya miji na vijiji ni eneo moja. lakini  katika utekelezaji wa  MDGS mapengo mengine hujitokeza. Ni kwa sababu hii hapana shaka kuwa  haki za binadamu  na utawala wa sheria ni  viwezeshaji  muhimu vya maendeleo” akasema.
Katika  kusisitiza  umuhimu wa  haki za binadamu na utawala wa sheria katika  kuwapatia wananchi maendeleo endelevu.  Wiziri anatoa mfano kwa kusema ni jambo lisilokubalika kwamba karibu watu   nne  bilioni wanakosa haki zitokanazo na  kutoka utawala wa sheria. Huku watoto saba kati ya kumi katika nchi  zilizonyuma kimaendelo hawana vyeti vya kuzaliwa.
Waziri Migiro anaongeza kuwa “ katika nchi nyingine uwiano kati ya  jaji  na idadi ya watu unasimama katika jaji  moja kwa watu  milioni. Ili hali katika nchi nyingine,  watu wanaendelea kubaguliwa kwa misingi ya  makabila yao, dini au jinsia. Haya yote Mwenyekiti yanaonyesha umuhimu wa  suala la haki za binadamu na utawala wa sheria kuwa sehemu ya maendeleo endelevu baada ya  2015”. 


Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Bw. Jan Eliasson akifungua majadiliano kuhusu mchango wa haki za  binadamu  na utawala wa sheria   katika kuunga mkono juhudi za kitaifa na  kimataifa  na nafasi yake katika suala zima la maendeleo endelevu baada ya  2015. Naibu Katibu Mkuu  alimtambulisha Waziri Migiro kama  mtangulizi wake na katika  hotuba yake alinukuu  baadhi ya  maneno ambayo Mhe. Migiro aliwahi kuyazungumza   kuhusiana na masuala ya  utawala wa sheria wakati huo akiwa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa  Mataifa.
 Muwakilishi wa  Kudumu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa  Balozi Tuvako Manongi,akifuatilia majadiliano kuhusu mchango wa haki za binadamu na utawala bora katika kusukuma mbele  suala zima la upunguzaji wa umaskini na  maendeleo endelevu.  Wachagizaji wakuu  wa majadiliano hayo alikuwa ni Mhe. Asha-Rose Migiro ( Mb) Waziri wa Sheria na Masuala ya Katiba, Bw. Christoph Strasser, Bw. Nicolas Lusian na Bw. Martin Kreutner.
Baadhi  ya washiriki wa majadiliano kuhusu mchango wa  haki za binadamu na utawala bora katika kuunga mkono juhudi za kitaifa na kimataifa kuelekea upunguzaji wa umaskini na maendeleo endelevu wakimsikiliza  Waziri wa Sheria na  Masuala ya Katiba Dk. -Rose Migiro ( Mb)

Chapisha Maoni

0 Maoni