Unordered List


KAMA HAUJAFATA TARATIBU HIZI BASI UMILIKI WAKO WA SIMU SI HALALI

TARATIBU ZA KUZINGATIA, KUWA NA WAMILIKI HALALI WA LAINI ZA SIMU


Na Eleuteri Mangi-MAELEZO
Mwanadamu ameumbwa na kuzaliwa akiwa na asili ya kuwa na uwezo na upeo unaomuwezesha kuwasiliana baina ya mtu na mtu kunzia ngazi ya familia, jamii inayomzunguka, taifa na hatimaye ulimwengu mzima.
Akiwa na mamlaka ya kutumia mawasiliano katika maisha yake ya kila siku, mwanadamu anayatumia mawasiliano hayo kama mchakato wa kuhamisha na kupashana taarifa ama habari kutoka sehemu moja hadi nyingine kwa nyakati tofauti tofauti.
Mchakato huo wa mawasiliano unaweza kuwa ni mwingiliano unaohusisha ishara kati ya angalau wakala wawili walio na mkusanyiko wa ishara na sheria za elimu ishara.
Kwa mantiki hiyo, mwanadamu anatumia mawasiliano kwa kupasha au kubadilishana mawazo, maoni, au habari kwa kunena, maandishi, au ishara.
Historia inasema, mawasiliano yamekuwepo tangu kuwepo mwanadamu hatua inayoleta mantiki kuwa mawasiliano yamekuwa kongwe kama jamii ilivyo kwani yamekuwepo tokea enzi za mababu.
Mwanadamu anatumia mawasiliano katika kutekeleza majukumu yake ya kila siku kulingana na wakati husika.(Martha Magessa)
Ndani ya mchakato wa kuhabarisha, habari husika hupakiwa, kutumwa na kupashwa na anayetuma kwa anayepokea kupitia kwa njia maalum kulingana na mahali na wakati husika.
Mawasiliano yakishatumwa, anayepokea hupakua ujumbe ule na kumpatia aliyetuma jibu ama majibu ya alichotaka kujulishwa ambapo mawasiliano yanahitaji anyetuma ujumbe na anayepokea wapate mrejesho unaoonesha kumekuwa na mawasiliano sahihi kulingana na mtoa ujumbe.
Ili kuwa na mawasiliano yenye tija katika jamii, njia zinazohusika na kusikia, kama vile unenaji, wimbo, na toni ya sauti, na zile zisizohusisha kusikia, kama vile miondoko ya mwili, lugha ishara, kugusa, kuwasiliana kwa macho, na kuandika.
Njia hizi husaidia jamii kupata ujumbe kwa kutumia ishara husika ambazo zinatarajiwa kuwa ni za kiungwana na zinazojali maadili ya kijamii na hivyo kuwa na taifa linalojitofautisha na mataifa mengine.
Mawasilano haya yanaweza kufikishwa kwa kutumia njia ya mdomo ama mazungumzo ya ana kwa ana, njia ya simu, radio, televisheni, intaneti na mitandao ya kijamii ambayo imekuwa ni njia ya haraka ya kupashana habari mbalimbali miongoni mwa jamii.
Kwa kwa suala la mawasiliano lilivyo nyeti kwa taifa, Serikali imetambua umuhimu huo na kutoa tahadhari kwa watumiaji wa huduma za mawasiliano, wananchi na umma kwa ujumla kwa kuwatahadhari watumiaji hao wa huduma hiyo nchini.
Matumizi mabaya ya mawasiliano na udanganyifu katika usajili wa namba za simu za mkononi imeonekana kuwa ni tatizo nchini ambapo hivi karibuni Serikali iliwatahadharisha wananchi kuhusu suala hilo na kuonya kuwa kutumia simu isiyosajiliwa ama kusajiliwa kwa kutumia taarifa za udanganyifu ni kosa la jinai.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es salaam Meneja mawasiliano wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) Innocent Mungy alisema kuwa kumekuwepo na watu wachache miongoni mwa jamii wanaotumia mawasiliano pasipo kuzingatia sheria na kanuni zilizowekwa nchini.
Ikizingatiwa TCRA ni chombo cha Serikali kilichopewa jukumu la kusimamia masuala ya mawasiiliano nchini, Mamlaka hiyo ilianzishwa kwa sheria. 12 ya mwaka 2003 kusimamia Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta nchini.
Ili kuendana na wakati, mwaka 2010, Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilipitisha Sheria la Mawasiliano ya Elektroniki na Posta (EPOCA) kusimamia, pamoja na mambo mengine, uuzaji, usajili na matumizi ya laini za simu za mkononi nchini.
Kwa kuwa TCRA jukumu lake ni kusimamia mwasiliano nchini, imekuwa mstari wa mbele mara zote kuwatahadharisha na kuwakumbusha wananchi kwa ujumla waitambue sheria hiyo ambayo imeainisha makosa yanayotokana na kukiuka vipengele vya sheria ya mawasiliano.
Miongoni mwa makosa hayo ni pamoja na kuuza au kusambaza laini ya simu bila kibali cha mtoa huduma za simu na kuwa na leseni kutoka TCRA na kutumia laini ya simu ambayo haikusajiliwa.
Makosa mengine ni kutoandikisha taarifa sahihi za laini husika kabla ya kuitoa au kuiuza, kutoa taarifa ya uwongo au maelezo yasiyo sahihi wakati wa kusajili laini ya simu na kuchakachua simu ya mkononi au laini ya simu.
Mnamo Mei 30, 2013 Mkurugenzi Mkuu Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania Prof. John Nkoma kupitia taarifa yake kwa vyombo vya habari aliwataka watumiaji wa simu za mkononi na wananchi kwa ujumla wa waunge mkono juhudi zinazofanywa na Serikali ili kufanikisha usajili wa namba za simu kwa ajili ya kudumisha na kuendeleza amani na usalama na kuharakisha maendeleo ya sekta ya mawasiliano na ya Taifa kwa ujumla.
Zoezi la kusajili laini za simu, lilikuwa na nia jema ambalo lilimtaka mteja mtarajiwa kusajili laini ya simu kwa kutoa taarifa sahihi kwa kuonesha mojawapo ya vitambulisho halisi vyenye picha yake ikiwemo hati ya kusafiria (Passport), kitambulisho cha kazi, leseni ya udereva, kadi ya usajili wa mpiga kura, barua ya utambulisho kutoka Serikali za Mitaa ikiwa na picha, kitambulisho cha Taifa, kitambulisho cha SACCOs au kadi ya benki yenye picha ya mhusika halisi anayetaka kusajili laini ya simu.
Haya yote Serikali imeyaweka ili kuzingatia na kuhakikisha kunakuwa na wamiliki halali wa laini za simu ili kurahisisha mawasiliano miongoni mwa jamii.
Kwa kuwa binadamu ni mrahisi kuelewa na ni rahisi pia kusahau, Serikali imweweka sheria ambayo iawakumbusha watumiaji wote wa mawasiliano kuwa yeyote atayekiuka Sheria hiyo ya Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta (EPOCA) ya mwaka 2010, kifungu cha 131, sheria hiyo imeainisha kuwa ni kosa la jinai kutumia au kuwezesha kutumika namba ya simu isiyosajiliwa kihalali.
Kutokana na kosa hilo, atakayebainika anatumia laini ambayo haijasajiliwa atakumbana na adhabu ya faini ya shilingi 500,000 au kifungo cha miezi mitatu ambayo itatolewa kwa yeyote atakayekiuka sheria hiyo.
Tahadhari zote hiyo inalenga na kuwashauri watumiaji wa simu za mkononi na wananchi kwa ujumla wawe tayari kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Serikali ili kufanikisha usajili wa namba za simu kwa ajili ya kudumisha na kuendeleza amani na usalama na kuharakisha maendeleo ya sekta ya mawasiliano na ya Taifa kwa ujumla.
Ni jukumu la letu sote kama wananchi kuzingatia matumizi sahihi ya mawasiliano kwa maslahi mapana yenye tija kwa umma na Taifa.
Aidha, Katika vikao vya pamoja na wadau wa mawasiliano nchini vilivyofanyika Aprili 04 na Aprili 11, 2013, Serikali kupitia Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania na makampuni yanayotoa huduma za simu za mkononi walikubaliana juu ya hatua za kumaliza kabisa tatizo la usajili wa namba za simu na utaratibu wa kufungia namba zote za simu ambazo hazikusajiliwa.
Vikao hivyo vyote viliwahusisha TCRA kwa upande wa Serikali, Watendaji Wakuu na wawakilishi wa mitandao ya Airtel, BOL, MIC (TIGO), Sasatel, TTCL, Vodacom na Zantel nchini.
Kwa mujibu wa kifungu cha 130 cha sheria ya Mawasiliano ya Elektroniki na Posta (EPOCA) ya mwaka 2010, sheria haijambana mtumiaji wa huduma tu, kwa upande mwingine imewataka wauzaji au wanaotoa kwa namna yoyote ile namba za simu bila kuzisajili ambapo akibainika atakuwa ametenda kosa la jinai.
Sheria imeainisha kuwa adhabu ya kutenda kosa hilo ni kulipa faini ya shilingi 3,000,000 au kifungo cha miezi 12 au adhabu zote zinaweza kutekelezwa kwa pamoja.
Ili kuhakikisha mawasiliano nchini yamekuwa yenye tija na yamekuwa kichocheo cha maendeleo, Serikali iliona kuna haja na sababu za msingi za kuanzisha utaratibu wa kusajili namba za simu na kupata taarifa sahihi za watumiaji wake.
Lengo mahususi likiwa kuwalinda watumiaji na jamii kutokana na matumizi mabaya ya huduma za mawasiliano, kuimarisha usalama wa taifa pamoja na kuwawezesha watoa huduma za mawasiliano kuwafahamu vizuri wateja wao na kuwahudumia ipasavyo kadiri ya mahitaji yao.
Zaidi ya hapo, Serikali pamoja na makampuni yanayotoa huduma ya mawasiliano waliona ni vema kuwezesha kuwatambua watumiaji wa huduma za ziada za simu, kama huduma za kibenki, kutuma na kupokea fedha, kufanya malipo mbalimbali kwa kutumia simu kwa mfano kulipia huduma za maji, umeme na vipindi vya televisheni vya kulipia.
Licha ya mawasiliano kuwa na mabadiliko kadiri ambavyo wakati umepita, teknolojia imeendelea kukua na kuibua aina mpya na mawazo kuhusu mawasiliano.
Maendeleo haya ya kiteknolojia yalibadilisha jinsi mawasiliano yanavyofanyika ambapo watafiti wamegawanya mawasiliano jinsi yalivyobadilika katika hatua tatu.
Mabadiliko ya mwanzo katika Mawasiliano yalibainisha kuwa maandishi na michoro ndiyo yalianza kutumika kuwasiliana.
Maandishi hayo yaliandikwa kwenye mawe, ambayo yalikuwa mazito mno kuhamishwa. Wakati huo, mawasiliano katika maandishi hayangeweza kubebwa, ingawa yalikuwepo.
Mabadiliko ya pili katika Mawasilianoyalihusisha maandishi ambayo yalianza kutumiwa kwenye karatasi, mavunjo, udongo na nta.
Herufi za alfabeti zilibuniwa, hivyo kuruhusu mfanano wa lugha katika maeneo makubwa, ilikuwa ni hatua kubwa baada ya muda, Mjerumani Johannes Gutenberg aliyeishi kati ya miaka ya 1398-1468, mwaka 1439 alikuwa mtu wa kwanza duniani kutumia mashine ya kuchapisha magazeti chini ya shirika aliloliita Gutenberg lililojihusisha na uchapishaji ili kurahisisha mawasiliano.
Ili kuhabarisha watu, shirika la Gutenberg lilitayarisha kitabu cha kwanza cha kuchapishwa kwa kutumia mashine yake ambapo maandiko haya yaliweza kusafirishwa kwa watu wengine duniani ili wayaone ambayo sasa mawasiliano hayo ya maandishi yanaweza kuhifadhiwa na kubebwa ikiwemo magazeti na vitabu.
Mabadiliko ya tatu ya Mawasiliano yalihusisha taarifa ambayo inaweza kuhamishwa kupitia mawimbi na ishara za kielektroniki ambayo duniani ndio hatua ya juu iliyopo ambapo mwanadamu anajivuni mabadiliko ya sayansi na teknolojia.
Kwa kuwa Tanzania ni miongoni mwa mataifa ya dunia ya leo imefikia kiwango cha watu wake kuweza kupata taarifa na kuhamishwa kupitia mawimbi, na ishara za kielektroniki zilizofikiwa kisayansi duniani, Serikali imeona ni vema iendelee kutoa tahadhari kwa watu wake ili wawe salama wakati wote.
Yanapotokea mafanikio katika jamii, wapo wanaotokea kuhujumu mafanikio hayo ndio maana Serikali kwa kuwajali watu wake imewasisitiza wananchi kujihadhari na utapeli unaoweza kufanywa kupitia simu za mkononi na mtandao wa intaneti.
Tahadhari hiyo iliyotolewa na Serikali inasisitiza kutokutekeleza maagizo yoyote yanayohusu fedha kwa ujumbe wa maandishi hata kama yanatoka kwa mtu unayemfahamu, mmliki wa simu kutumia namba ya siri ambayo sio rahisi mtu mwingine kukisia na kutokutoa namba za siri za anazotumia mmiliki wa simu katika masuala yanqayohusu miamala ya kifedha.
Tahadhari nyingine ni kutokutekeleza maagizo yoyote kutokana na ujumbe wa simu za mkononi unaomtaka mtumiaji wa simu kutuma fedha kutoka namba ambayo mtumiaji wake unamfahamu na ambao unakueleza kuwa simu yake inahitilafu, hivyo hawezi kuongea, usitekeleze maagizo hayo.
Zaidi ya hayo, mtumiaji wa simu anatakiwa kutumia namba ya siri ambayo sio rahisi mtu mwingine kuikisia, kutokutoa namba za siri anazotumia mteja wa simu na kuhakikisha namba ya mtu unayemtumia pesa au salio kabala ya kutuma.
Aidha, mmliki wa simu akipoteza simu yake au laini anapaswa kutoa taarifa kwa mtoa huduma aliyeko karibu nae na aende polisi mara moja kutoa taarifa hiyo.
Endapo mteja asipopata ushirikianaoa wa kutosha kwa mtoa huduma aliyeko karibu yake, mteja anapaswa kuwasilisha malalamiko hayo kwa TCRA.
Njia sahihi za kufikisha malalamiko ni pamoja na kuyatuma kwa kuandika Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania, S. L. P. 474 Dar es salaam ama kufika ofisi za TCRA makao makuu Dar es salaam au ofisi za kanda na Zanzibar.
Namana nyingine ni kupiga simu namba 0784558270 au 0784558271 na kwa barua pepe malalamiko@tcra.go.tz aucomplaints@tcra.go.tz .
Pamoja na baadhi ya tahadhari hizo, Serikali inaendelea kuweka mazingira mazuri kwenye Sekta ya Mawasiliano ambayo yameonesha inaendelea kukua nchini na imekuwa na matokeo makubwa.
Kadiri siku zinavyokwenda, kumekuwa na idadi ya kubwa ya watumiaji wa huduma za mawasiliano nchini.
Idadi hiyo imeendelea kuongezeka kutoka laini za simu za kiganjani milioni 2.96 mwaka 2005 hadi kufikia milioni 27.45 mwezi Desemba 2013 ambapo watumiaji wa mfumo wa intaneti nao wameongezeka kutoka milioni 3.56 mwaka 2008 hadi kufikia milioni 9.3 mwezi Desemba 2013.
Vilevile, mawasiliano nchini yanavyozidi kuongezeka, kumekuwa na ongezeko kubwa la huduma kupitia mawasiliano ya simu za kiganjani ambapo huduma za kifedha zinazotolewa kwa watumiaji wa simu hizo zimeongezeka pia.
Katika kudhihirisha hilo, Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia Prof. Makame Mnyaa Mbarawa (Mb), katika hotuba yake wakati akiwasilisha Bungeni makadirio ya mapato na matumizi ya fedha kwa mwaka 2014/2015 mwezi Mei mwaka huu alisema kuwa huduma zilizoongezeka ni pamoja na miamala ya kifedha ambayo ina watumiaji wapatao 12,330,962 na ununuzi wa huduma na bidhaa kwa kutumia miamala ya kibenki.
"Hivi sasa, wananchi wanaweza kufanya malipo ya huduma mbalimbali wanazozitumia kupitia simu za kiganjani" alisema Prof. Mbarawa.
"Katika kipindi cha Julai, 2013 hadi Aprili, 2014 kuna jumla ya miamala 972, 641,605 yenye thamani inayofikia shilingi Trilioni 28.3 imefanyika", aliongeza Prof. Mbarawa.
Prof. Mbarawa alisisitiza kuwa maendeleo hayo yamesaidia kuokoa muda wa wananchi na kupunguza msongamano sehemu za kulipia na kupata huduma hizo wanazohitaji kwa wakati bila usumbufu wowote.
Maendeleo hayo ndiyo yanayoisukuma Serikali kupitia TCRA kujiwekea malengo katika mwaka wa fedha 2014/2015 ambayo itatekeleza kwa kufanya tathmini ya gharama za huduma za simu za mkononi na kufanya utafiti kuhusu utoaji wa huduma za intaneti na matumizi ya masafa yanayowezesha mawasiliano ya intaneti (Broadband) ili yaboreshwe na kufikia wanachi wengi zaidi na kupata mawasiliano yenye tija manufaakwa taifa.
Aidha, alipokuwa akihitimisha hotuba yake, Prof. Mbarawa aliyashukuru makampuni ya simu za kiganjani kwa kuwa tayari katika kushughulikia changamoto za mawasiliano katika maeneo yasiyo na mawasiliano hapa nchini.
Mbali na huduma ya mawasiliano, Prof. Mbarawa alisema kuwa makampuni hayo ya simu nchini yamekuwa tayari katika kuchangia maendeleo na upatikanaji wa huduma za jamii zenye tija kwa wananchi.
Makampuni hayo yameonesha nia ya dhati na kushiriki katika shughuli mbalimbali za kijamii kama vile uchangiaji wa damu salama, ujenzi wa vituo vya afya, ununuzi wa vitabu vya ziada na kiada vinavyotumika mashuleni na vyuoni, ununuzi wa madawati na ujenzi wa madarasa.
Tukiwa kwenye ulimwengu wa utandawazi, kama nchi ni vema kusimamia maadili ya Kitanzania na utamaduni wetu mwema unayoipambanua nchi yetu na mataifa mengine kwa kuzingatia misingi ya utaifa wetu.
Tuyatumia mawasiliano kama sekta muhimu nchini ili taifa lifikie malengo yake ya kuwa nchi ya uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.
Maenedleo hayo hayawezi kufikiwa kama Watanzania wote kwa umoja wao, nchi na mashirika ambayo ni washirika wa maendeleo, watatumia vibaya mwasiliano kwa lengo la kubomoa badala ya kujenga.
Hima hima TCRA, jukumu mlilopewa na taifa la kusimamia mawasiliano ni nyeti, juhudi zenu zisonge mbele ili watumiaji visivyo wa mawsiliano wachukuliwe kuwa ni wahujumu maendeleo ya taifa letu.
Ni suala la kiungwana na la kisheria kwa watumiaji wa simu za kiganjani kusajili namba zao za simu mbapo TCRA mara zote inawahimiza kusajili laini zao za simu.
Ili kujihakikishia kuwa laini yako ya simu imesajiliwa ni vema mtumiaji wa simu husika kuthibitisha na kijiridhisha kama usajili wake upo sahihi kwa kupiga *106# kwenye simu yako.
Uhakiki huo unahusisha watumiaji wa huduma ya mawasiliano kupitia mfumo wa makampuni ya Vodacom, Airtel, Tigo na Zantel, SASATEL na TTCL Mobile, na watasikiliza maelekezo.
Taarifa utakayoipata inatakiwa kutaja jina lako kama mtumiaji halali wa namba husika, na iwapo utapata jibu tofauti, tafadhali fika kwenye ofisi ya mtoa huduma wako au wakala wake ili kurekebisha kasoro hizo.
Watumiaji wa simu za mkononi na wananchi wanashauriwa kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Serikali ili kufanikisha usajili wa namba za simu kwa ajili ya kudumisha na kuendeleza amani na usalama na kuharakisha maendeleo ya sekta na ya Taifa kwa ujumla.

Chapisha Maoni

0 Maoni