Ndugu Zangu,
Najisikia
furaha katika siku hii ya leo kuwaona vijana wale wa Burkinafaso, kwa
kuamua kuingia mitaani wamemlazimisha Blaise Compaore kuachia ngazi.
Siku hii
ya leo inanikumbusha Jumamosi moja mwaka 1990. Nilikuwa Kidato cha Sita
pale Sangu Sekondari. Vijana tuliandaa debate kwa Kiingereza. Nilipata
nafasi ya kusimama jukwaani kumzungumzia Mwanamapinduzi Captain Thomas
Sankara. Pale ukumbini tulikuwa na Emmanuel Nchimbi pia. Namkumbuka pia
Alfred Mwambeleko. Captain Sankara alikuwa Rais kijana, Mjamaa na
mwanamapinduzi. Nakumbuka ziara yake ya kwanza baada ya kuchukua
madaraka ilikuwa Tanzania kuonana na Mwalimu.
Huko
nyuma nimepata kutoa mifano kadhaa ya viongozi walioacha hiba nyuma yao,
hiba njema na mbaya; nilimtolea mfano Captain Thomas Sankara. Kuwa
aliacha hiba njema ya kuenziwa ndani ya nchi yake, Afrika na duniani.
Mwanamapinduzi
huyu alikuja kuawa kwa kupigwa risasi na wapinga mapinduzi na maendeleo
ya Burkina Faso. Na aliyempindua ni Blaise Compaore, rafiki yake.
Sankara alipata kukaririwa akisema;(P.T)
"Ningependa
kuacha nyuma yangu, imani ya kuwa, kama tunaimarisha kiwango fulani cha
uangalifu na oganaizesheni, basi, tunastahili ushindi. Kamwe huwezi
kuleta mabadiliko ya kimsingi bila ya kuwa na kiwango fulani cha
uwendawazimu.
Hali hii inatokana na kutoshinikizwa na taratibu zilizozoeleka, kuwa na ujasiri wa
kuzipa mgongo kanuni za kizamani, ujasiri wa kuanzisha mustakabali.
Ni wendawazimu wa jana waliotuwezesha kuyafanya tuyafanyao leo.
Ninataka kuwa mmoja wa wendawazimu hao." ( Hayati, Kapteni Thomas Sankara)
0 Maoni