Waziri
Mkuu, Mizengo Pinda akizungumza na Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro
Nyalandu (wapili kushoto) na Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu,
Aggrey Mwanri (kulia) baada ya kufunga Mkutano wa kupiga vita ujangili
wa wanayamapori na kuendeleza uhifadhi wa wanayamapori mjini Arusha
Novemba 8, 2014. Kushoto ni Mbunge wa Kahama, James Lembeli.Wapili kulia
ni Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki, Dkt Richard
Sezibara(Picha na ofisi ya Waziri Mkuu)
........................................................................................
* Ataka iundwe timu kufuatilia utekelezaji wa Azimio la Arusha 2014
WAZIRI
MKUU Mizengo Pinda amesema inahitajika dhamira ya kweli kutoka kwa wadau
wote katika kutekeleza Azimio la Arusha la kukabiliana na ujangili na
kuendeleza hifadhi za wanyama katika nchi za Afrika Mashariki na zilizo
Kusini mwa Ikweta.
Akizungumza
na waandishi wa habari jana jioni (Jumamosi, Novemba 8, 2014) mara
baada ya kufunga mkutano wa kikanda wa siku mbili uliojadili mbinu za
kupambana na biashara haramu ya wanyamapori ulioandaliwa na Wizara ya
Maliasili na Utalii jijini Arusha, Waziri Mkuu alisema: "Suala hili
linataka uwajibikaji wa pamoja. Mashirika na taasisi, wananchi na
viongozi sote kama wadau wakuu, kila mmoja anapaswa kushiriki vita hii
kama kweli tunataka tuitokomeze."
"Kwenye
hili Azimio la Arusha na nyie waaandishi wa habari pia mna sehemu yenu
mmetajwa... wamesema wanatafuta jinsi ya kushirikiana na vyombo vya
habari ili visaidie kutoa elimu kwa jamii kama njia ya kuelimisha umma,"
alisema.
Waziri
Mkuu aliwaeleza waandishi hao kwamba Azimio hilo lina vipengele 20
ambavyo vinataka utekelezaji katika ngazi ya nchi mojamoja, ngazi na
kanda na ngazi ya kimataifa kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo.
"Nimepata
faraja kwamba mkutano huu haukuisha kijumlajumla tu, bali umekuja na
maazimio 20 ambayo yametengwa kwa ajili yetu sisi wa ndani, mengine
yanahusisha ushirikiano wa kikanda na yako mengine yanawahusisha wadau
wa maendeleo," alifafanua.
Ili
kutekeleza azimio hili, nimeshauri iundwe timu itakayoshirikisha vyombo
vingi zaidi badala ya kuiachia Wizara ya Maliasili na Utalii peke yake.
Timu hii ikutane kila baada ya miezi sita ili kufuatilia utekelezaji wa
maazimio haya na ikibidi Waziri atoe taarifa bungeni kuhusu utekelezaji
huo," alisema Waziri Mkuu.
Mapema,
akizungumza na washiriki wa mkutano huo wakati wa kuufunga, Waziri Mkuu
alisema kuwepo kwa watu wa ngazi tofauti kwenye mkutano huo ni kielelezo
tosha cha umakini wao na nia thabiti ya kutokomeza ujangili katika
ukanda huu.
"Tumeanzisha
vita, tusisahau kwamba bado kuna kazi kubwa mbele yetu na vita
haijaisha. Tuzidishe mapambano katika sehemu tatu: kwenye nchi
unakofanyika ujangili, nchi ambazo nyara zinapitishwa na nchi
zinazopokea ama kununua hizo nyara," alisema Waziri Mkuu.
"Nakubaliana
nanyi kwamba hakuna nchi inayoweza kukabili suala la ujangili ikiwa
peke yake. Tunahitaji tuwe na sera mahsusi, sera ya pamoja ya
kutuunganisha na kutuongoza wakati tukitekeleza Azimio hili kwa
kusaidiana na wadau wa maendeleo," alisema.
Alisema
Azimio hilo litaipa kazi ya ziada ya Wizara ya Maliasili na Utalii
ambapo kazi kubwa itakuwa ni kusimamia na kuhakikisha utekelezaji wa wa
Azimio hilo unakuwa wa ufanisi.
Jumla ya
nchi tisa zimetia saini azimio hilo mbele ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.
Nchi hizo ni Burundi, Kenya, Uganda, Msumbiji, Tanzania, Sudan Kusini,
Zambia, Rwanda na Malawi.CHANZO FULL SHANGWE
0 Maoni