Unordered List


VIONGOZI TANZANIA SAFI ICC-MEMBE

UMOJA wa Afrika (AU) unatarajia kukutana hivi karibuni kujadili hatua za kuchukua kutokana na Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta kupandishwa kwenye Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai (ICC) hivi karibuni.Hatua hiyo inatokana na kupuuzwa kwa ombi la AU la kutaka Marais wa Afrika kutofikishwa ICC.Katika hatua nyingine, imeelezwa kwamba viongozi wa Tanzania hawatafikishwa katika mahakama hiyo, kujibu mashitaka yoyote, kutokana na kufanya kazi nzuri na kwa kuzingatia misingi ya utawala bora na haki za binadamu.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, alisema bungeni mjini hapa jana kuwa viongozi wa nchi za Afrika, watajadili hatua za kuchukua dhidi ya ICC katika kikao chao kitakachofanyika Addis Ababa, Ethiopia Januari mwakani.

Rais Kenyatta alipandishwa katika Mahakama hiyo iliyopo The Hague, Uholanzi, Oktoba 8, mwaka huu, pamoja na Azimio la Umoja wa Afrika, kutaka viongozi wa Afrika wasifikishwe katika mahakama hiyo wanapokuwa madarakani.
Viongozi hao wa nchi za Afrika, walifikia Azimio hilo katika mkutano wao uliofanyika Addis Ababa, Ethiopia, Oktoba 2013.
Akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Chwaka, Yahya Kassim Issa (CCM) aliyehoji hatua zitakazochukuliwa na AU kwa Rais Kenyatta kupandishwa kizimbani na ICC, Membe alisema nchi 34 za Afrika wanachama wa ICC watatoa uamuzi wao kwa kitendo hicho.
Alisema pia kuwa si rahisi kwa viongozi wa Tanzania kufikishwa katika mahakama hiyo, kwa vile wanaendesha nchi vizuri na kwa kuzingatia misingi ya utawala bora.
“Naomba nilihakikishie Bunge kwamba hakuna kiongozi wa Tanzania atakayefikishwa ICC maana wanaendesha nchi vizuri sana,” alisema Membe.
Awali akijibu swali la mbunge huyo, Waziri Membe alisema ni kweli kwamba katika miaka ya hivi karibuni imejitokeza hali ya baadhi ya viongozi wa nchi za Afrika kushitakiwa ICC, lakini kushitakiwa huko hakumaanishi kuwa nchi za Afrika hazina umoja.
“Kimsingi nchi za Afrika zina umoja ulio imara. Hii inathibitishwa na namna nchi za Afrika zilivyoonesha umoja na mshikamano wa kiwango cha juu katika kukabiliana na changamoto hii. “Kupitia AU nchi za Afrika zimefanya vikao na kupitisha maazimio na maamuzi ya pamoja kwa ajili ya kupinga kushitakiwa kwa viongozi wa nchi za Afrika walio madarakani katika Mahakama hiyo ya ICC na kuliomba Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lenye mamlaka ya kusitisha kesi hizo kufanya hivyo,” alisema Membe

Chapisha Maoni

0 Maoni