Unordered List


KATIBU MKUU WA UVCCM NDUGU SIXTUS MAPUNDA AWALIPUA CHADEMA, ADAIWA KUNYAKA TAARIFA ZA SIRI ZA MIPANGO YA VURUGU SIKU YA KUPIGA KURA.

Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) na mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (M-NEC) Ndugu Sixtus Mapunda amesema kuwa Chadema wamepanga njama haramu za kuvuruga uchaguzi wa Serikali za mitaa kwa kuwaandaa vijana wa kufanya vurugu na kuwazuia akina mama na wazee wasiende katika maeneo ya kupigia kura.
Mapunda ameyasema hayo leo majira ya saa tano na nusu asubuhi wakati akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Mwanzugi Kata ya Igunga , mkoani Tabora ambako yupo katika ziara ya Kikazi ya siku kumi na nne katika mikoa ya Tabora, Shinyanga, Geita na Kagera.
“..tumepata taarifa za kuaminika kuwa Chadema wameandaa vijana na kuwaandalia viroba na bangi ili waweze kufanya vurugu siku ya uchaguzi na kuwazuia wananchi kwenda kupiga kura katika vituo vilivyoandaliwa.,tunawataka waache mpango huo mara moja kwani vyombo vya dola viko macho na vitawachukulia hatua wote watakaofanya hujuma hizo..”

alisema Mapunda katika mkutano wa hadhara uliofanyika eneo la Mwanzugi stendi na kuhudhuriwa na mamia ya wakazi wa kijiji cha Mwanzugi.

Pia, Mapunda amewataka wananchi kuwachagua Viongozi wanaotokana na Chama Cha Mapinduzi kwani ni waaminifu, wakweli na wenye anuani kamili kwa maana ya kuwa wanazo ofisi zinazotambulika katika kila kijiji na Kata ambako wananchi wanaweza kupeleka malalamiko yao na kusikilizwa tofauti na vyama vingine ambavyo havina ofisi wala anuani ya Kudumu.

Mapunda ameendelea na mikutano yake ya hadhara katika Mkoa wa Tabora ambako anatarajia kuzungumza na wananchi wa wilaya za Kaliua, Urambo na Nzega.

Chapisha Maoni

0 Maoni