AKIWA
katika maadhimisho ya kuanza mwaka wa pili wa utume wake katika kuongoza
Kanisa Katoliki Duniani, Baba Mtakatifu Francis, ametoa kauli kuashiria
kuwa huenda asidumu katika wadhifa huo kwa muda mrefu ujao.
Alisema
hayo juzi katika mahojiano ya ana kwa ana na kituo kimoja cha
televisheni cha Mexico, Televisa News, baada ya kutangaza kuwa Desemba
mwaka huu, Kanisa Katoliki litaadhimisha Mwaka Mtakatifu.
Mwaka huo
Mtakatifu utaanzia Desemba 8, mwaka huu na kuisha Novemba 20, mwakani.
Inaelezwa kuwa kuzinduliwa kwa Mwaka Mtakatifu au Jubilee, kunaendana na
maadhimisho ya 50 ya kufungwa kwa Baraza la Pili la Vatican, ambalo
hukusanya maaskofu ambao huzungumzia mambo ya baadae ya kanisa.
Mwaka huo
Mtakatifu utakuwa wa 29 tangu utaratibu huo ulivyoanza mwaka 1300. Kwa
kawaida Mwaka Mtakatifu huadhimishwa kila baada ya miaka 25.
Ukomo
wake Katika tamko hilo, Baba Mtakatifu Francis mwenye umri wa miaka 78,
ameweka wazi kuwa hataadhimisha miaka mingine mitakatifu katika siku
zijazo. “Nina hisia kwamba utume wangu utakuwa wa muda mfupi, kama miaka
minne au mitano; sijui inaweza hata kuwa miwili au mitatu lakini miaka
miwili imeshapita,” alitabiri katika mahojiano hayo.
Hata
hivyo, hakutaka kuweka wazi kama atafuata nyayo za mtangulizi wake, Baba
Mtakatifu mstaafu Benedict XVI, ambaye ameweka historia ya kuwa Baba
Mtakatifu wa kwanza kustaafu katika miaka 600 iliyopita, baada ya
kuchukua hatua hiyo mwaka 2013.
Alipoulizwa
swali mahususi kama atafuata nyazo za Baba Mtakatifu mstaafu, Benedict
XVI, alijibu; “Huenda Benedict XVI akabakia kuwa Baba Mtakatifu mstaafu
pekee kwa miaka mingi ijayo, na huenda akapata mwenzake,” na kuongeza
kuwa Baba Mtakatifu mstaafu “ameonesha njia.” Hii si mara ya kwanza kwa
Baba Mtakatifu Francis kuzungumzia ukomo wake, kwa kuwa amewahi kusema
kustaafu kwa Baba Mtakatifu Benedict XVI mwaka 2013, kusichukuliwe kuwa
tukio la pekee.
Pia,
alisema hakuchukia kuteuliwa kuwa Baba Mtakatifu, lakini aliweka wazi
kwamba katika wadhifa huo, amejikuta akipoteza uhuru wake. “Natamani
tena kuwa na uwezo wa kutoka nje siku moja bila mtu yeyote kunifuatilia
na kunitambua nikajinunulie mahitaji yangu,” alisema na kutabasamu.
Lengo la
mahojiano hayo na kituo hicho cha Televisa News, lilikuwa kujadili
maisha yake ikiwemo mawasiliano yake na baadhi ya watu, ambao wamekuwa
wakimwandikia barua kumshirikisha katika huzuni zao na kupata ushauri
wake.
Umasikini,
wahamiaji Baba Mtakatifu pia alizungumzia hali ya uhamiaji duniani na
kuibuka kwa wimbi la wakimbizi wanaokimbia umasikini, njaa na vita
katika nchi zao za kuzaliwa.
Katika
mahojiano hayo yaliyochapishwa katika kurasa 17, Baba Mtakatifu Francis
alisema kwa kuwa yeye ni Baba Mtakatifu wa kwanza kutoka Bara la Amerika
ya Kusini, analazimika kuzungumzia wahamiaji na watu masikini kwa
sababu babu zake walihama kutoka Italia kwenda Argentina kutafuta kazi.
“Watu
wamekuwa wengi bila kazi, kiasi cha kulazimika kutafuta kazi mahali
pengine,” alisema Baba Mtakatifu Francis, ambaye safari yake ya kwanza
baada ya kuteuliwa kushika wadhifa huo, alitembelea kisiwa cha
Lampedusa, Italia kutoa heshima kwa maelfu ya wahamiaji waliokufa
wakijaribu kwenda katika Bara la Ulaya. CHANZO: HABARI LEO
0 Maoni