Dar es
Salaam: Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mwadhama
Polycarp Kardinali Pengo amesema waumini hawana budi kusoma vizuri na
kuelewa Katiba Inayopendekezwa ili wakati ukifika, wafanbye uamuzi kwa
hiari na utashi wao wakati wa kupiga Kura ya Maoni.
Ametoa
kauli hiyo ikiwa ni siku mbili baada ya Jukwaa la Wakristo kutoa tamko
linalowataka waumini kujitokeza kwa wingi kujiandikisha kwenye Daftari
la Wapigakura, kushiriki kikamilifu kwenye shughuli zote za elimu ya
Katiba Inayopendekezwa na kupiga kura ya "hapana" kuikataa Katiba
Inayopendekezwa.
Lakini
jana, Kardinali Pengo alisema kuisoma na kuielewa katiba hiyo ndiyo
wajibu wa msingi ambao Wakristo wanao kwa sasa ili kupiga kura
inayostahili wakati ukifika. Kuhusu maaskofu kuagiza waumini waikatae
Katiba Inayopendekezwa, Kardinali Pengo alisema wao wakiwa viongozi wa
watu, hawana mamlaka wala uwezo huo, bali wenye uwezo ni wananchi
wenyewe.
Hata
hivyo, Kardinali Pengo alitaka tamko hilo lisambazwe kwenye parokia na
vigango vyote vya Jimbo Kuu la Dar es Salaam ili waumini wasomewe,
wauelewe kwanza, ili hatimaye waweze kufanya uamuzi sahihi wakielewa ni
nini wanachokitakiwa kukifanya.
Changamoto za familia
Katika
hatua nyingine, Kardinali Pengo pia alizungumzia changamoto za wanandoa,
ikiwamo tabia ya kuchepukia nje ya ndoa ambayo alisema inasababisha
amani kutoweka ndani ya familia.
Akizungumza
katika ibada ya Kwaresima kwa Wanawake Wakatoliki Tanzania (Wawata)
jana, Kardinali Pengo alisema akina mama wengi kwa sasa, hususan katika
ndoa wamekuwa wakisaliti ndoa na baadaye kuwatupia lawama watoto wao juu
ya tabia walizoanzisha wenyewe.
Katika
mahubiri yake aliyoyatoa katika Kanisa la Mt. Joseph Dar es Salaam,
mbali na changamoto sugu za kifamilia, Kardinali Pengo alijikita katika
kuangalia aina sita za malezi kwa watoto na athari za utandawazi kwenye
jamii.
"Wapo
wanawake ambao kwa sasa wanaendekeza michepuko kwenye familia na
wamekuwa hawana hofu ya Mungu wakati wote. Kuna wengine ambao wanavaa
mavazi ya mabinti wakisema wanakwenda na wakati," alisema.
"Wanawakemea watoto wao wakati wao wanaendekeza tabia chafu, wakiulizwa wanasema eti wao wameshakuwa watu wazima."
Katika
sehemu ya mafundisho yake, mbali na kupungua uaminifu, Kardinali Pengo
alizitaja changamoto nyingine alizosema kuwa zimeendelea kuumiza familia
ambazo ni tofauti za kiimani, kipato, elimu, kulea watoto nje ya ndoa,
kushindwa kudhibiti maadili ya watoto, ushirikina na ufisadi.
Alisema changamoto hizo zinatafuna familia nyingi kwa sasa.CHANZO: MWANANCHI
0 Maoni