Mbunge wa
Bumbuli ambaye pia ni Naibu Waziri Sayansi na Teknolojia, January
Makamba akipokelewa na wazee mara baada ya kuwasili jimboni kwake.
Mbunge wa
Bumbuli ambaye pia ni Naibu Waziri Sayansi na Teknolojia, January
Makamba akipokelewa na akina mama na kupewa baraka zake.
Na Raisa Said, Bumbuli.
Wakazi
mbalimbali wa Jimbo la Bumbuli, wilayani Lushoto, Mkoani Tanga wamesema
kuwa wapo tayari kumuunga mkono Mbunge wa Jimbo hilo, January Makamba
kama ataamua kuwania nafasi ya kuwa mgombea wa Uraisi wa CCM katika
Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka huu. Wakazi hao ambao walionyesha nia yao
hiyo katika sehemu mbalimbali alizopita Mbunge huyo katika ziara yake ya
siku sita kutembelea jimbo lake iliyoanza Machi 30. Makamba ni
mmojawapo wa watu wanaotajwa kuwania nafasi hiyo ya Urais.
Alipokuwa
katika kata ya Tamota, viongozi wa dini walimfanyia maombi maalum
ambayo yaliongozwa na Mchungaji Amasia Mweta na Sheikh Amiri Yahaya
Shekibula mara baada ya kumalizika kwa mkutano wa hadhara uliohutumbiwa
na Mbunge huyo kijana. Akihutubia mamia ya wakazi wa Bumbuli katika
maeneo yote aliyopita kwenye ziara yake, Makamba aliwashukuru wakazi wa
jimbo hilo kwa kumchagua kuwa Mbunge wao na kusema kama sio wao
asingeweza kuonekana na kutajwa katika kuwania nafasi ya kuwa mgombea wa
CCM.
Makamba,
huku akishangiliwa na wakazi hao wa maeneo hayo, alisema kuwa hakuna
namna ambayo unaweza kutengeneza watu kukutaja katika nafasi za juu bila
kupitia kwa wananchi kukuchagua katika nafasi ya kuwawakilisha.
"Kutajwa si dhambi na kwa kuwa fomu za uchaguzi sio sumu si dhambi pia
kuchukua na kuingia katika kinyang'anyiro hicho," alisema na kuongeza
kuwa sasa hivi kuna kiu kubwa ya uongozi wa aina mpya na kuna watu
wamemuona na kumtaja yeye jambo ambalo si baya.
Nao
wananchi , wakiwemo vijana, kina mama na wazee katika maeneo mbalimbali
aliyopitia Makamba, walimhakikishia Mbunge huyo kuwa hivi sasa
hawatampokea mtu yeyote ambaye atakuja kujipitisha katika jimbo hilo
hadi hapo watakapojua hatma ya utekelezaji wa nia ya Mbunge huyo kuwania
nafasi ya kuwa mgombea wa Urais kupitia CCM. Nao waumini wa Usharika wa
Bumbuli walimtaja Mbunge huyo kuwa jasiri, mweledi na mwenye maono
mapana na wakasema wanaahidi kuwa bega kwa bega katika harakati hiyo ya
kuwania kuwa mgombea wa CCM.(Muro)
0 Maoni