Unordered List


UVCCM WATOA POLE KWA WAATHIRIWA NA TETEMEKO LA ARDHI

TANZIA  YA UVCCM KWA UMMA KUFUATIA TETEMEKO LA ARDHI  HUKO BUKOBA MKOANI KAGERA TAREHE 10 SEPTEMBA 2O16.

Kufuatia  kutokea janga la tetemeko la Ardhi huko Bukoba  Mkoa Kagera ambalo limepoteza maisha ya watu kadhaa, kuharibu mali na makaazi ya wananchi , Jumuiya ya Vijana ya CCM (UVCCM )tumepokea kwa huzuni na masikitiko makubwa .

Umoja wa Vijana ya Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) tumepokea kwa  mshituko  mkubwa tukio hilo kubwa na zito  ambalo  limesababisha kutokea kwa maafa na  hasara ya mali na makaazi ya watu.

Tukio hilo lililotokea  siku mbili zilizopita limeacha misiba, majeruhi na watu kupoteza mali , vitu vyao vya thamani na kuharibu  maakazi ya binadamu ambao  sasa hawana uhakika wa makaazi mengine.

Janga hilo licha ya kuleta majonzi  vile vile limeathiri maisha ya watu  kinadharia na kisaikolojia ikiwemo watu kupata hofu ya maisha yao, limepoteza nguvu kazi ya Taifa yaani vifo na majeruhi wakiwemo vijana, wanawake na watoto .

Katika kipindi hiki kigumu Jumuiya yetu inaungana  bega kwa bega na watanzania wengine kwa kuzipa mkono wa pole familia zote zilizopoteza ndugu zao na pia tukiwafariji wale wote waliopata hasara ya kuharibikiwa nyumba zao na kupoteza mali.

Janga hili ni letu wote, limemgusa kila mtanzania mwerevu mwenye upendo na uzalendo , lazima litukusanye na kutukutanisha tukiwa wamoja ili kuyakabili magumu yote yaliotokea kwa wakati huu.

Tukio hili la kimaumbile ya dunia huwa na athari kubwa, linapotokea  huleta kiza cha misiba na kurudisha nyuma juhudi za watu waliojijenga kimaisha kwa kupoteza mali na rasilimali zao

Tunampa mkono wa pole Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk John  Pombe Magufuli kwa tukio hili zito linaloambatana na vifo vya watanzania wenzetu.

Tunawaomba watanzania wenzetu, ndugu na jamaa ambao wamepoteza ndugu zao, watoto na jamaa zao wawe wenye moyo wa subira katika  wakati huu mgumu na wenye huzuni kubwa .

Tunamuomba mungu awepe ustahamilivu, mioyo yao mungu aitie subira na stahamala huku nasi kwa umoja wetu tutakuwa pamoja wakati wote ili kusaidiana na wenzetu ambao wamepata matatizo hayo.

Tunawashukuru na kuwakupongeza viongozi wenzetu  walioko katika maeneo husika  wakiongozwa na Mwenyekiti wa Vijana wa CCM wa Mkoa wa Kagera Ndg Yahya Kateme  makundi mbali mbali ya vijana yaliyojitokeza kutoa mashirikiano makubwa wanayoendelea  katika janga hili kwa hakika wametuwakilisha vyema vijana wote wa Tanzania nasi kwa mapenzi ya Mwenyezimungu tutafika kuungana nao katika kuwafariji na   kutoa misaada ya kibinadamu.

Huu si wakati wa siasa bali ni kipindi kigumu cha kukabili yale yote yaliotokea na kudhuru au kuharibu taaswira iliokuwepo awali ya ustawi wa maisha ya wenzetu ambao wamepatwa na janga hilo.

Kila kijana mzalendo ni vyema akaenda kuripoti kwa viongozi wa maeneo husika aidha wakuu wa wilaya au mkoa ili kupewa maelekezo na miongozo katika kila hatua ya kusaidiana kwa hali na mali wakati wote hadi hali itakaporejea kama kawaida.

Mungu Ibariki Tanzania. Mungu Ibariki Afrika na watu wake wote.

Ahsanteni

SHAKA HAMDU SHAKA (MNEC)

Kaimu Katibu Mkuu.

Chapisha Maoni

0 Maoni