Unordered List


MPANGO WA KUINUA UBORA WA ELIMU NCHINI WAENDELEA MKOANI SIMIYU

Mpango wa Kuinua Ubora wa Elimu nchini (MKUE-T), ukishirikiana na Sekretarieti ya Mkoa wa Simiyu pamoja na Halmashauri sita za mkoa huo, wanashiriki katika maonyesho ya wiki ya vijana kitaifa yanayoendelea mkoani humo.

Lengo kuu ni kuwafikia wananchi wengi ili waweze kufahamu Mpango wa Kuboresha Elimu unafanya nini katika maeneo yao hasa kwenye nyanja za;
  • Kuboresha utendaji kazi wa walimu kupitia mafunzo ya walimu kazini.
  • Kuimarisha uongozi na usimamizi wa shule kwa kutoa mafunzo kwa Waratibu Elimu Kata, Walimu wakuu na Walimu wakuu wasaidizi.
  •  Kuimarisha usimamizi wa mipango ya kielimu katika ngazi ya Halmshauri kwa kuwajengea uwezo maafisa wasimamizi wa elimu katika ngazi ya Wilaya na Kata.
  • Kuimarisha ushiriki wa jamii katika maendeleo ya elimu; uwazi na uwajibikaji wa jamii katika kuzijengea uwezo kamati za shule, uanzishwaji wa ushirikiano wa wazazi na walimu, kuijengea jamii uwezo kutambua na kuanisha mahitaji ya kielimu na kupanga mipango ya kielimu inayotekelezeka.
  • Kuimarisha mfumo wa ukusanyaji, utunzaji na usambazaji wa taarifa za kielimu na uwajibikaji. Wananchi wamejitokeza kwa wingi kwenye banda la elimu kujifunza jinsi mpango huu unavyotekelezwa ukilenga kuinua ubora wa elimu katika mkoa wa Simiyu.

Wanafunzi/watoto wengi wamejitokeza kuangalia zana za kufundishia na kujifunzia zilizotengenezwa na walimu pamoja na walimu wasaidizi wa jamii, na kujisomea vitabu vya hadithi, Wazazi nao wanaendelea kujitokeza kujifunza zaidi hususani wajibu wao kama wazazi katika kuboresha elimu katika maeneo yao na watoto wao kwa ujumla.

Akizungumza juu ya alichojifunza, mzazi Minza Masunga, alisema, “ mwanzoni nilikuwa najua jukumu langu kama mzazi linaishia katika kumnunulia mtoto vifaa vya shulle tu, na walimu ndio wenye jukumu la kuhakikisha mtoto anajua kusoma na kuandika pamoja na kufaulu vizuri, lakini kupitia mpango huu nimeelewa mimi kama mzazi nina jukumu kubwa katika kuboresha elimu”.
Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini akipata maelekezo kutoka kwa Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Girikwe B, Mwalimu Samwel Mandu kuhusu taarifa zinazohusiana na walimu, wanafunzi na miundo mbinu ya shule zinavyoingizwa katika mfumo wa taarifa.
Mratibu wa kituo cha Walimu Busega, Bi. Faidha Habibu akiwasikiliza watoto wakisoma vitabu vya hadithi.
Afisa Elimu Taaluma wa Wilaya ya Maswa, Mwalimu Genoveva Gerard akiwaelimisha wanawake waliotembelea juu ya ushiriki wa wananchi katika kuchangia maendeleo ya elimu katika maeneo yao.
Mratibu wa Elimu Kituo cha Walimu Wilaya ya Bariadi, MwL Rose Nyanduru akimueleza mwananchi kuhusu vituo vya utayari, na zana zinazotengenezwa kwa ajili ya watoto.
Walimu wasaidizi wa vituo vya utayari wakitoa elimu kwa wananchi juu ya madarasa ya Elimu ya Awali na zana za kufundishia na kujifunzia.
Afisa Elimu Taaluma wa Wilaya ya Maswa, Mwl. Genoveva Gerard akimsikiliza mtoto akisoma kitabu cha hadithi
Mratibu wa Elimu Kata akiwaelezea wananchi juu ya Mpango wa Kuinua Ubora wa Elimu nchini.
Watoto wakiangalia baadhi ya zana za kufundishia na kujifunzia watoto wa vituo vya utayari wa kuanza shule.

Chapisha Maoni

0 Maoni