Unordered List


NAIBU WAZIRI JAFO AWAFAGILIA WATENDAJI NA VIONGOZI TEMEKE KWA KUTEKELEZA MAAGIZO YA SERIKALI

Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Tawala za mikoa na serikali za mitaa(Tamisemi), Selemani Jafo amewapongeza viongozi na watendaji wa wilaya ya Temeke kwa kutekeleza maagizo yake aliyoyatoa mwezi mmoja aliopita ikiwa ni pamoja na kuhakikisha wanafunzi wanakaa kwenye madawati na kuongezwa vyumba vya madarasa.

Mnamo mwezi Septemba mwaka huu, Jafo alizitembelea shule nne za wilaya ya Temeke zilizopo eneo la mbagala na kukutana na changamoto lukuki, zikiwemo kutotembelewa shule hizo na Afisa elimu wilaya toka mwaka huu uanze kitendo kilicho sababisha kutobainika kwa changamoto ili zipatiwe ufumbuzi.

Shule alizozitembelea ni pamoja na shule za msingi Chemchem, Nzasa, Charambe, na Kilamba ambapo Jafo alikuwakuta watoto wa darasa la saba pekee kwa shule ya Chemchem ndio waliokuwa wakikalia madawati.Katika shule ya nzasa, Naibu Waziri huyo aliwakuta watoto wamejazana huku kukiwa hakuna mpango wowote wa ujenzi wa madarasa.

Aidha aliwakuta walimu wakiwa hawana ofisi ya walimu licha ya shule hizo kuwa katika jiji la biashara lenye mapato mengi.Hata hivyo, Shule ya Kilamba pekee ndiyo ilikuwa katika hali ya kuridhisha, na baada ya ziara hiyo alitoa maagizo kwa mkurugenzi wa Temeke kuzifanyia kazi changamoto alizo zibaini kwa kipindi cha mwezi mmoja.

Jafo alifanya tena ziara kwenye eneo hilo ili kubaini utekelezaji wa maagizo yake na katika safari hiyo ya pili alifanikiwa kuzitembelea shule alizozitembelea awali pamoja na shule mbili nyingine za Kiburugwa na Kingugi.Alipofika alikuta watoto wote wakiwa katika madawati pamoja na kuanza kwa harakati za kuongeza madarasa na ujenzi wa ofisi za walimu kwa shule hizo ambazo baadhi zilikuwa hazina.

Kadhalika, Mkurugenzi wa Manispaa ya Temeke, alimpa taarifa Jafo kuwa shule ya Nzasa itapata jumla ya vyumba saba, Chemchem vyumba vitano, chalambe vyumba vinne na ofisi ya walimu na kilamba kujengewa fensi ya shule.Naibu Waziri huyo aliwashukuru na kuwapongeza viongozi wote wa temeke kwa kujali matatizo ya jamii.

Katika ziara hiyo Jafo aliongozana na Mkuu wa wilaya ya Temeke, Mbunge wa jimbo la Mbagala Issa Mangungu, Meya ya Temeke Chaurembo, Mkurungenzi wa Manispaa ya temeke na wakuu wake wa idara huku akisema viongozi hao ni mfano wa kuigwa.

Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na serikali za mitaa, Selemani Jafo akizungumza na walimu na wanafunzi wa shule ya msingi Kilamba, kushoto ni Mbunge wa Mbagala, Issa Mangungu.

Chapisha Maoni

0 Maoni