WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa
amesema Serikali imetenga fedha nyingi kwa ajili ya ununuzi wa dawa na
vifaa tiba na kwamba hakuna mgonjwa atakayekwenda kutibiwa katika
hospitali, vituo vya afya au zahanati bila ya kupatiwa dawa.
Ameyasema hayo jana jioni
(Jumatatu, Julai 10, 2017), wakati akizungumza na wananchi wa wilaya ya
Liwale katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Uwanja wa Michezo wa
Wilaya.
Waziri Mkuu ambaye ameambatana na
mkewe Mama Mary Majaliwa katika ziara yake ya kikazi ya siku nne Mkoani
Lindi, alisema Serikali haitaki kusikia wananchi wanakwenda hospitali,
Vituo vya afya au zahanati na kukosa dawa.
Alisema moja kati ya ajenda
muhimu ya Serikali ya awamu ya Tano ni kuboresha huduma za afya kwa
wananchi wake, ambapo kila mwezi halmashauri zote nchini zinapelekewa
fedha za ununuzi wa dawa.
“Serikali hii ya Rais Dkt. John
Magufuli inatoa fedha za kununulia dawa kila mwezi katika halmashauri
zote nchini. Sasa kama hapa Liwale kuna malalamiko ya wananchi kukosa
dawa katika hospitali yetu, Mkuu wa Wilaya kafuatilie huko Halmashauri
ili kujua wanapeleka wapi fedha za dawa.”
Katika bajeti ya Wizara ya Afya,
Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ya mwaka wa fedha 2017/2018
jumla ya shilingi bilioni 236 zimetengwa kwenye ununuzi wa dawa, vifaa,
vifaa tiba na vitendanishi.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa
Lindi, Bw. Godfrey Zambi alisema hali ya upatikanaji wa dawa muhimu kwa
kipindi cha mwaka 2016/2017 iliongezeka kwa asilimia 50 ikilinganishwa
na ile ya mwaka 2015/2016.
Bw. Zambi alisema katika kipindi
cha kuanzia Julai mwaka 2016 hadi Februari 2017 mkoa wa Lindi ulipokea
sh milioni 538 kwa ajili ya ununuzi wa dawa kupitia Bohari ya Dawa
(MSD).
“Hospitali ya mkoa ilipokea sh.
milioni 195,328,186 kwa ajili ya ununuzi wa dawa na pia ilitumia sh.
Milioni 127,171,700 toka fedha za uchangiaji kwa ununuzi wa dawa.”
Katika hatua nyingine, Waziri
Mkuu aliwaagiza watendaji wa Halmashauri kwenda vijijini na kuwaelimisha
wananchi umuhimu wa utunzaji wa mazingira ili kuliepusha Taifa kugeuka
jangwa.
Pia amewaagiza Maofisa Kilimo
wote kuhakikisha wanaacha kushinda maofisini na badala yake waende
mashambani kwa ajili ya kuwaelimisha wakulima namna bora ya kulima kwa
kufuata njia za kisasa ili kupata tija.
Kila ofisa kilimo awe na shamba lake ambalo litatumika kama darasa kwa wananchi
0 Maoni