Unordered List


SHAKA AKUMBUSHA JAMBO LA MAANA


Na Mwandishi wetu
 Emmanuel J. Shilatu.

Kaimu Katibu Mkuu Umoja wa Vijana Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Ndugu Shaka Hamdu Shaka alifanya ziara ndefu katika mikoa ya Kigoma na Mwanza. Akiwa ziarani mkoani Mwanza, Ndugu Shaka alikumbushia juu ya wajibu wa halmashauri zote kuhakikisha wanatoa asilimia 10 ya mapato yake kwa mgawanyo wa asilimia 5 kwa vijana na asilimia 5 kwa Wanawake kwa ajili ya mikopo kama ilivyobainishwa kwenye ilani ya Chama Cha Mapinduzi.

Hayo yamesemwa na Kaimu Katibu Mkuu wa UVCCM Taifa Ndg Shaka Hamdu Shaka (MNEC) Wilayani Ilemela Mkoani Mwanza Wakati wa ziara ya siku moja alipokuwa akizungumza na Vijana wa Jumuiya ya Chama hicho (UVCCM) pamoja na  wanachama wa chama cha Mapinduzi (CCM) katika mkutano wa ndani uliofanyika katika Uwanja wa CCM Kirumba.

Shaka alisema kuwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kinafahamu kuwa Changamoto kubwa ya Vijana nchini ni ukosefu wa ajira lakini Serikali inayoongozwa na Chama Cha Mapinduzi inaendelea kutumia njia Mbalimbali ikiwemo kuwashauri Vijana Kujiunga na vikundi Mbalimbali vya ujasiriamali ili wapatiwe mikopo waweze kujiajiri wenyewe.

"Nitakuwa muongo kama nitasema sifahamu changamoto zinazowakabili Vijana wengi kiuchumi kwa wale waliopo ndani ya Chama Cha Mapinduzi ama wale waliopo nje ya CCM lakini Serikali inayotekeleza ilani yetu ya ushindi ya Mwaka  2015 imeeleza vyema namna bora ya kuwasaidia Vijana kujiajiri" Alisema Shaka.

Kwanza kabisa nimpongeze Ndugu Shaka kwa kufanya ziara ya kihistoria iliyojaa mwamko na hamasa kubwa sana ya ujenzi wa jumuiya ya Vijana. Tumejionea wenyewe kwenye vyombo vya habari na mitandao ya kijamii uwingi wa watu kwenye ziara yake na namna mamia ya Watu wakijiunga na CCM  ambapo walikabidhiwa kadi za CCM  na Ndugu Shaka.

Pili; Katika ziara hiyo Ndugu Shaka aliitumia kuhakikisha anawapa elimu ya ujasiliamali jambo ambalo ni tija tosha kwa vijana kuweza kukabiliana na tatizo la ajira nchini. Nampongeza kwa hilo pia.

Ni ukweli ulio wazi kuwa kuna tatizo kubwa la ajira nchini. Na hii sio Tanzania tu bali duniani kwa ujumla. Nchini Tanzania tatizo la ajira linawaathiri haswa kundi la vijana ambao wengi wao hawana ajira rasmi yaani ajira za kuajiliwa.

Mathalani asilimia 15 ya vijana wenye sifa ya kuajiriwa nchini wanakabiliwa na tatizo la ajira. Kumekuwa na shida kubwa kwenye ajira rasmi kwa maana fursa ni chache kulingana na uwingi wa idadi ya wahitaji. Ajira pekee iliyopo ni ya kujiajili.

Tatizo hili limeonwa na Serikali na limebainishwa wazi wazi kwenye ilani ya Chama Cha Mapinduzi, ambayo Serikali iliyopo madarakani inaizingatia. Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015, Ibara ya 59 inazielekeza Mamlaka za Serikali za Mitaa zote nchini kuzingatia viashiria vya ukuzaji ajira katika mipango ya maendeleo ya ngazi husika pamoja na kutoa taarifa za mwenendo wa ajira kila robo mwaka.

Mamlaka ya Serikali za mitaa kupitia Manispaa zimeweka utaratibu wa kutenga asilimia 10 ya mapato yake kuhakikisha wanawapa mikopo vijana ya asilimia 5 na Wanawake asilimia 5 kupitia vikundi rasmi vilivyosajiliwa kisheria. Lakini jambo la kushangaza ni kuwa manispaa nyingi hazizingatii kabisa juu ya agizo hilo.

Zipo baadhi ya Manispaa hazitengi kabisa fungu hilo, Manispaa nyinginezo zinatenga pesa hizo lakini haziwafikii walengwa bali huishia mifukoni mwa wajanja wachache na kuacha kundi kubwa la vijana na wanawake wakiwa kwenye shida, tabu na karaha ya msoto wa maisha kutokana na kukosa ajira.

Manispaa zilizo nyingi hutumia mikopo hii kama fursa yao ya ulaji ambapo baadhi ya madiwani hutumia fursa hii kuzila ama kuwapa watu wanaowataka wao wenyewe pasipo kufuata taratibu za kisheria . Badala ya pesa hizi kuwa mkombozi, zimekuwa kero na lawama tele kwa jamii.
Kitendo cha Ndugu Shaka kuwakumbusha Manispaa juu ya kutekeleza wajibu wao wa lazima wa kutenga asilimia 5 (5%) na wahakikishe zinawafikia kweli vijana husika. Hii ndio maana halisi ya kuwa kiongozi, kuwa sauti ya wengi kwa manufaa ya wengi.

Ni lazima Manispaa zielewe kuwa tatizo kubwa la ajira nchini na ajira pekee mkombozi kwa vijana na wanawake ni ajira za kujiajili. Hauwezi kujiajili kama hauna mtaji wa kuweza kujiajili. Vijana wakienda kwenda kwenye taasisi za kifedha kuomba mikopo wanapewa masharti magumu yanayomshinda kijana kuyamudu. Unakuta kijana anaambiwa apeleke hati ya nyumba, au hati ya shamba, au aonyeshe biashara aliyonayo iwe dhamana yake! Mambo hayo yote kwa kijana wa kawaida hawezi kuyapata kiurahisi.

Njia pekee nyepesi ya kijana kuweza kupata mtaji ni kupitia mikopo ya fedha za asilimia 5 zinazotoka Manispaa ambazo Wakurugenzi wameamliwa kuzitenga na kuwapa vijana lakini hawafanyi hivyo. Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa wanapaswa kuliona hili kwa jicho pana zaidi na kuwabaini wale wote wanaokwamisha utekelezwaji wa agizo hilo na kuwapa adhabu kali iwe fundisho kwa wote wanaokwamisha maagizo ya Serikali kuu, iwe fundisho kwa wote wanaohujumu utekelezwaji wa ilani ya uchaguzi ya CCM.

Tunaziona jitihada za dhahiri za Serikali za kupambana na tatizo la ajira nchini kwa kuhakikisha wanaboresha kilimo nchini kwa kuhakikisha pembejeo zinapatikana kwa wakati, uboreshwaji wa vipimo kwa kuondoa rumbesa, kodi za mazao ya kilimo zinafutwa. Mathalani, Serikali imefuta kodi kwenye mazao ya korosho, pamba na n.k

Serikali imeendelea kujenga na kuboresha miundo mbinu ili kuweka uwepesi bidhaa kutoka na kufika masokoni kiurahisi. Kila mtu anaona namna namna ambavyo barabara zinavyojengwa, treni ya kisasa inavyojengwa kwa hadhi ya standard gauge ambayo itakuwa na uwezo mkubwa pamoja na spidi kali zaidi.

Katika kutatua tatizo la ajira nchini tumeona namna ambavyo Serikali ya awamu ya tano ilivyojikita kwenye ujenzi wa viwanda vya kisasa nchini. Mathalani, ndani ya mwaka mmoja, jumla ya viwanda 2,169 vimesajiliwa vikiwemo viwanda vya mbolea, saruji, chuma na vya usindikaji wa mazao.

Ili kuendelea kuvutia uwekezaji nchini. Uhamasishaji wa ujenzi wa viwanda nchini ni dhahiri na tayari tumeanza kuona matokeo. Kwa mfano, mkoa wa Pwani peke yake una viwanda vikubwa 83 na vingine vidogo vidogo zaidi ya 200. Hakika hii ni Tanzania ya viwanda.

Kiukweli kwa upande wa Serikali imejitahidi sana kuhakikisha wanapunguza kama sio kuondoa kabisa tatizo la ajira nchini. Hata hii ya kuhakiki wenye vyeti na majina feki ni sehemu ya kupambana na walioziba fursa halali za wenye vigezo ndio maana hivi sasa ajira nyingi zimetangazwa kwenye sekta mbalimbali na hivyo kuwapa vijana wasomi fursa ya kuajiriwa. Hakika, huu ni mkakati mzuri wa Serikali wa kupunguza idadi ya wasio na ajira nchini. Tatizo kubwa lipo kwenye manispaa zetu ambazo hazitengi asilimia 10 za vijana na Wanawake.

Nampongeza sana Kaimu Katibu Mkuu UVCCM, Ndugu Shaka kwa kuonyesha dhahiri kukerwa na tatizo la ajira nchini, kukerwa na ubabaishaji unaofanywa na Manispaa katika kuwapatia mikopo stahiki Vijana na Wanawake ili waweze kujiajili na kujikwamua kimaisha. Tanzania inahitaji viongozi kama Shaka wenye mitazamo mipana zaidi ya kuona njia za kuwanasua vijana kwenye matatizo ya ajira nchini.

Chapisha Maoni

0 Maoni