Unordered List


KITUO CHA UWEKEZAJI TANZANIA(TIC) YAKANUSHA TAARIFA YA ILIYOTOLEWA NA GAZETI YA FINANCIAL TIMES KUWA SERA ZA UWEKEZAJI TANZANIA ZINAKIMBIZA WAWEKEZAJI


Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania Ndg. Geoffrey Mwambe amesema kwamba taarifa zilizotolewa na Mwandishi wa FT. John Aglionby kuhusu mazingira ya Uwekezaji Tanzania kuwa yanatishia wawekezaji si sahihi na yanalenga kupotosha ukweli kuhusu hali halisi kuhusu Uwekezaji Tanzania.

Mwandishi huyo wa Financial Times ametoa maelezo ambayo amesema yametolewa na Muwekezaji Aliko Dangote maelezo ambayo yamelenga kusukuma Agenda yake ambayo haijulikani na yenye lengo la kupotosha sera za uwekezaji na kuwaogopesha wawekezaji ambao wameendelea kuiamini Tanzania na kuwekeza mitaji yao mikubwa hapa nchini.

Hatuamini kuwa Ndugu Dangote anaweza kuwa msemaji wa kuhusiana na sekta ya madini kwa hapa nchini. Amewekeza kwenye sekta ya viwanda na serikali imekuwa mstari wa mbele kusikiliza na kuyafanyia kazi maoni ya mfanyabiashara huyo ili kuweza kuboresha mazingira yetu ya uwekezaji hapa nchini. Serikali yetu imejidhatiti katika kuboresha mazingira ya uwekezaji na imedhamiria kuhakisha uwekezaji huo unakuwa na faida kwa watanzania nan chi kwa ujumla.

Tunaamini kuwa kuna umuhimu wa kuhakikisha maelezo yanakuwa na pande mbili ili kuondoa utata utaojitokeza wa maelezo ambayo yanaweza kuathiri na kusababisha utata kwa wafanyabiashara walioiamini Tanzania kama sehemu yao ya kufanya uwekezaji. Tanzania inathamini na kujali wawekezaji wa aina ya ya Aliko Dangote na mara nyingi tumekuwa tukiwasikiliza na kufanyia kazi maoni yao ili kurekebisha sera ili ziweze kuwa na manufaa kwa wote yaani waTanzania na wawekezaji. Kuna sera pamoja na sheria ambazo tumezifanyia marekebisho ili ziweze kuwa na manufaa kwa wote.

Hivi karibuni ni vizuri kufahamu kwamba DIL ilikuwa na matatizo mbalimbali na serikali iliweza kukaa na Dangote na kusikiliza matatizo yao na kutatua changamoto kadhaa zilizokuwa zinakwamisha uzalishaji katika kiwanda chake cha Saruji na kufikia muafaka wa kutatua matatizo yote ambayo kiwanda ilikuwa ina TIC pia imeanzisha juhudi maalum za kuhakisha kuwa huduma zinotolewa kwa wawekezaji zinaboreshwa ili kuweza kurahisisha utoaji wa huduma kwa ufanisi na kwa haraka. Kituo kimeweza kuanzisha Kamati Maalum ya Kitaifa ya Kuhudumia wawekezaji yaani NIFC ambapo matokeo makubwa yameweza kuonekana kutokana na uboreshwaji wa huduma zetu chini ya mahali pamoja .

Tunamshukuru sana Mh. Rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania Dokta John Pombe Magufuli kwa juhudi zake za dhati za kupambana na rushwa juhudi ambazo zimeweza kuleta mafanikio n ahata kuifanya Tanzania kutajwa na ripoti mbalimbali za dunia kama mahala bora Zaidi pa kuwekeza Afrika. Zaidi ya ripoti tano zimeweza kuitaja Tanzania kwa mwaka huu pekee kama sehemu bora Zaidi ya mazingira ya uwekezaji Afrika. Tunajivunia juhudi kubwa sana alizozionyesha Rais wetu Mh.John Pombe Magufuli katika kuvutia uwekezaji nchini hasahasa katika kutokomeza rushwa, jambo ambalo mwandishi wa makala hiyo kwa sababu zake binafsi ameshindwa kuziweka bayana.

Ni muhimu sana kuelewa kuwa suala la kuwa na sera nzuri za uwekezaji kwa manufaa ya mwekezaji na nchi limepewa kipaumbele kikubwa na Serikali ya Awamu ya Tano. Tunahitaji sekta binafsi kutekeleza majukumu yake kwa kufuata sheria na taratibu, mfano kulipa kodi stahiki wakati Serikali kwa upande wake ikiendelea kuboresha zaidi mazingira ya biashara na uwekezaji nchini. Katika makala yaliyotolewa na FT imejionyesha waziwazi kuwa mwandishi hafahamu vizuri Sheri ya Uwekezaji ya Mwaka 1997.

Sheria za Tanzania zinatambua umiliki binafsi wa mali na kuzuia uwezekano wa kutaifisha mali hizo bila sababu za msingi za kisheria. Vilevile Tanzania ni mjumbe wa Multilateral Investment Guarantee Agency (MIGA) ambapo makubaliano ya wajumbe ni kutoruhusu utaifishwaji wa mali za uwekezaji pamoja na Kituo cha Kimataifa cha Usuluhishi wa Migogoro ya Kibiashara (ICSID).

Tanzania inaendelea kuhamasisha uwekezaji nchini na Kituo cha Uwekezaji kimekuwa mstari wa mbele katika kushawishi wawekezaji na mashirika makubwa ya kimataifa ambayo tayari yana uwekezaji nchini kuongeza mitaji yao. Tanzania imeendelea kupokea wawekezaji wengi ambapo uwekezaji huo umesaidia katika kukuza uchumi katika Nyanja mabilimbali mfano kuzalisha ajira mpya na kuongeza mapato ya kikodi. Matokeo haya chanya yanatokana na juhudi za Serikali kujenga mazingira mazuri ya biashara na uwekezaji nchini.

Mkurugenzi Mtendaji wa TIC amewashukuru wawekezaji waliowekeza mitaji yao Tanzania kwa ushirikiano wao mzuri na kuwaahidi kuwa Serikali itaendelea na juhudi zake za kuboresha mazingira ya uwekezaji ikiwa ni pamoja na kuboresha mfumo mzima wa kuwahudumia wawekezaji.

Ili kuhakikisha kuwa nchi yetu inaendela kuwa na mazingira mazuri ya uwekezaji, Serikali imeipa kipaumbele utekelezaji wa miradi ya miundombinu wezeshi ili kusaidia katika kupunguza gharama za uwekezaji. Baadhi ya miradi hii ni pamoja na Mradi wa kuzalisha umeme wa Stiegler’s Gorge, ujenzi wa barabara, ukarabati wa miundombinu ya Bandari ya Dar es Salaam (Gati 1-7), ujenzi wa Reli ya Kati kwa iwango cha standard gauge. Jitihada nyingine zilizofanyika hivi karibuni ni uanzishwaji wa Mfuko wa Benki ya Ardhi (Land Bank Fund) na kuboresha mfumo wa asajili wa makampuni BRELA.

Tanzania imeendelea kufanya vizuri kwenye kuvutia uwekezaji ukilinganisha na nchi nyingine za Jumuiya ya Afrika Mashariki. “Tanzania imo katika orodha ya nchi kumi bora Afrika zinazovutia uwekezaji kulingana na ripoti ya Rand Merchant Bank (RMB). Vilevile Tanzania imeendelea kuwa na kiasi kikubwa cha mitaji ya uwekezaji kutoka nje ya nchi (foreign direct investment) ukilinganisha na nchi nyingine za Jumuiya ya Africa Mashariki” amesema Bw.Mwambe

Chapisha Maoni

0 Maoni