Unordered List


HALMASHAURI YA ILALA YAAHIDI KUDUMISHA MIRADI DAR-URBAN







Katibu Tawala wa Halmashauri ya Ilala Ndugu Edward Mpogolo.

Halmashauri ya Wilaya ya Ilala jijini Dar es Salaam imeahidi kuendeleza na kudumisha miradi iliyoachwa na shirika la Plan International katika maeneo ya Buguruni na Vingunguti.

Ahadi hiyo imetolewa leo jijini humo na Katibu Tawala wa Halmashauri hiyo, Edward Mpogolo alipokuwa akifunga programu ijulikanayo kama Dar – Urban iliyoanzishwa na shirika hilo ambayo imedumu katika maeneo hayo kwa miaka 26.

Mpogolo amesema kuwa shirika hilo limefanya kazi nzuri tangu kuanzishwa kwa program hiyo kwani imeleta mapinduzi makubwa katika kuimarisha huduma muhimu kwa wananchi kwa kuboresha sekta mbalimbali zikiwemo za elimu, afya na ujenzi wa miundo mbinu.

“Toka mwaka 1992 wamekuwa na sisi wakitusaidia kutuboreshea huduma mbalimbali na katika kipindi chote hicho wameweza kutujengea shule mbili za msingi, kutujengea kituo cha Afya cha Buguruni, kuwaelimisha na kuwainua vijana hivyo tunawaahidi kuisimamia na kuidumisha miradi yote waliotuachia”, alisema Mpogolo.

Mpogolo amefafanua kuwa baada ya shirika hilo kujenga shule mbili za msingi za Vingunguti na Buguruni Moto Mpya mnamo mwaka 2016 ufaulu uliongezeka kutoka asilimia 49 mpaka asilimia 98 pia tangu walipojenga kituo cha afya mnamo mwaka 2002 wagonjwa walikuwa 40 mpaka 50 kwa siku lakini kwa sasa kituo kinapokea wagonjwa kati ya 500 mpaka 600.

Vile vile katika kuelimisha vijana, Mpogolo amesema kuwa shirika hilo linajitahidi kuendana na Sera ya Serikali nchini ya kuwasaidia vijana ambapo wameweza kuelimisha vijana zaidi ya 2,000 na vijana hao wametumika kuwaelimisha wenzao zaidi ya 29,000 walioweza kujianzishia shughuli zao binafsi kwa ajili ya kujikimu. 

Aidha, Mpogolo ametoa rai kwa shirika hilo kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma muhimu ambazo zitasaidia kupunguza utegemezi kati yao na kuwafanya waweze kuchangia katika kukuza uchumi wa nchi.

Kwa upande wake Meneja Miradi ya Dar – Urban kutoka shirika la Plan International, Nicodemus Gachu amesema kuwa progamu hiyo inafungwa baada ya kuhitimisha utekelezaji wa miradi mbalimbali hivyo watahamia katika maeneo mengine yenye uhitaji.

“Kwa miaka 26 mradi huu umetumia zaidi ya bilioni 15 katika kutekeleza miradi mbalimbali ya afya, elimu, ulinzi wa mtoto, ushirikishwaji, elimu ya afya ya uzazi na uwezeshaji vijana kiuchumi”, alisema Gachu.

Mradi huo utahamishiwa katika wilaya ya Nkasi iliyopo mkoani Rukwa kwa lengo kubwa la kumuwezesha mtoto wa kike kupata fursa mbalimbali katika jamii pamoja na kusaidia maeneo yenye uhitaji katika wilaya hiyo.

Chapisha Maoni

0 Maoni