Unordered List


MBUNGE JAMES MBATIA AHUSISHWA NA MATUMIZI MABAYA YA FEDHA ZA MFUKO WA MAENDELEO YA JIMBO LA VUNJO.



Mwanasheria Emmanuel Mlaki kutoka Wilaya ya Moshi amelalamikia kitendo cha Mbunge wa Jimbo la Vunjo Mhe. James Mbatia kutumia Fedha za Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo la Vunjo vibaya.

Katika maelezo yake Mwanasheria huyo amelalamikia kitendo cha Mbunge James Mbatia kutumia ushawishi wake kama Mbunge na Mwenyekiti wa kamati ya kupanga na kuratibu Fedha za Mfuko wa Maendeleo ya  Jimbo la vunjo kubadili Bajeti iliyopangwa hapo awali ya kupeleka pesa hizo za Serikali zipatazo kiasi cha Shilingi Milioni 45,908,878.00/=  katika maeneo yote yaliyopangiwa kupata mgawo huo wa Fedha za Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo la Vunjo kwa jumla ya Kata 12.

Kata hizo mbazo zilikuwa sehemu ya mgawo wa Fedha za Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo la Vunjo ni Marangu Mashariki, Makuyuni, Kahe Magharibi, Kilema Kusini, K/v/Magharibi, Marangu Magharibi, K/v/ Mashariki, Mamba Kusini, Mamba Kaskazini, Mwika Kaskazini, Njiapanda na K/v/ kusini. Kwa kutumia nafasi yake ya kiti alihakikisha pesa hizo za Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo la Vunjo  zaidi ya shilingi Milioni 30,000,000.00/=  sawa na asilimia 75% ya pesa zote kupelekwa katika Kata moja tu ambayo ni Marangu Mashariki kwa ajili ya ujenzi wa Barabara, ambao kimsingi ujenzi huo unasimamiwa na asasi isiyo ya serikali ijulikanyo Vunjo Development Foundation na tayari asasi hiyo ilishasimamishwa na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Moshi Mhe. Kippi Warioba kwa kufanya shughuli zake kwa kukiuka sheria na taratibu za nchi huku Kata zingine zilizopaswa kupata mgawo huo wa Fedha kuambulia shilingi 0/= sifuri.

Kitendo hicho ni kinyume na Sheria ya Mfuko wa Maendeleo wa Jimbo Kifungu cha 12 ya Mwaka 2009; “Orodha ya miradi inayoweza kutekelezwa inatakiwa kuibuliwa na wananchi wanaoishi katika Jimbo husika”. Mh. James Mbatia aeleze ni wananchi gani waliomwambia apeleke asilimia 75% ya fedha zote katika kata moja ya Marangu Mashariki kwa ajili ya kujenga Barabara zinazosimamiwa na asasi ya VDF!

Mwanasheria Emmanuel Mlaki amelalamikia kitendo cha  Mbunge wa Jimbo la Vunjo Mhe. James Mbatia kwa kitendo  chake cha kuwahadaa wananchi wa Jimbo la Vunjo kupitia mkutano wake wa hadhara alioufanya tarehe 25/11/2018 katika viwanja vya Himo Kata ya Makuyuni kwa ahadi ya kutoa pesa zake za mfukoni ili kurudisha umeme katika kituo cha polisi Himo na badala yake ameamua kutumia Fedha za Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo la Vunjo kiasi cha shilingi Milioni 5,000,000.00/= kinyume na taratibu.

Kitendo hicho ni kinyume na kifungu  Namba 10 cha Sheria ya Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo ya mwaka 2009 kinachotaka kila Kata kuandaa Miradi inayopewa kipaumbelena kuiwasilisha kwenye Kamati ya Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo kwa ajili ya kuidhinisha. Mh. James Mbatia awaeleze wanachi wa kata ya Makuyuni uhalali wa Kamati ya Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo la Vunjo kupeleka shilingi milioni 5 kwa ajili ya kulipia umeme  kituo cha Polisi Himo.? 

Mwanasheria Emmanuel Mlaki amepinga utaratibu mzima uliofanywa na kamati hiyo huku akimtaka Mhe. Mbunge James Mbatia na Afisa Mipango wa Halmashauri ya Wilaya ya Moshi kujipima upya kama wanatosha katika nafasi zao.

Pia, amemuomba Mkuu wa Wilaya ya Moshi Ndg. Kippi Warioba  na Mkurugenzi kuingilia kati suala hilo ambalo kuna ukiukwaji mkubwa wa utaratibu uliofanyika.

Chapisha Maoni

0 Maoni