Unordered List


UVCCM YAOMBOLEZA KIFO CHA FEROUZ

Atakumbukwa kwa mema aliyoitendea jumuiya.

  Na Mwandishi wetu Iringa

Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) umepokea kwa huzuni , masikitiko na fazaa taarifa ya kifo cha aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Saleh Ramadhan  Farouz aliyefariki usiku wa kuamkia leo na kuzikwa (adhuhuri) mchana huu  katika makaburi ya Mwanakwerekwe kisiwani Unguja.

Tanzia ya UVCCM iliyotolewa na  Kaimu Katibu Mkuu wa UVCCM Shaka Hamdu Shaka kwenda kwa Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi  (CCM )Kanali Mstaafu Abdulrahman Kinana Ofisi ndogo ya CCM Lumumba imeeleza kuwa kifo hicho ni pigo kwa  CCM na jumuiya zake.

Shaka alimueleza Kinana kwamba marehemu Ferouz ni zao la juhudi na maandalizi ya Chama cha Mapinduzi kwa vijana wake na kwamba utumishi wake toka akiwa UVCCM hadi kufikia  Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar kwa miaka kumi mfululizo ni kielelezo cha kutosha katika utendaji wake uliotukuka.

Amesema vyovyote itakavyokuwa kifo cha mwanasiasa huyo licha ya kuacha pengo ambalo litakawia kuzibika, atakumbukwa kwa tabia yake ya kupenda Umoja, muungano,  kujichanganya na kutopindisha maneno katika jambo lenye maslahi kwa Taifa.

"UVCCM tumepokea kwa huzuni na fazaa kubwa taarifa za kifo cha kada wa chama chetu, kiongozi jasiri na mwanasiasa mpiganaji shupavu kwa maslahi ya Taifa na mweledi katika uchambuzi wa masuala ya kisiasa "alisema shaka

UVCCM imeisihi familia yake, wana CCM na watanzania wapenzi wa Umoja , amani na mshikamano kuwa na subira, uvumilivu na utulivu katika wakati huu mgumu wa msiba na maombolezo .

"Yapo mambo mengi ya kujifunza unapoyatazama na kuiakisi safari ya kisiasa ya Saleh Ramadhani Ferouz katika maisha yake hadi kifo kumkuta, hatutaacha wala kubeza  lolote jema alilolifanya katika kipindi  cha uongozi wake na ushiriki wake katika maisha ya siasa"alisisitiza .

Shaka alisema UVCCM inaungana na familia ya marehemu katika kipindi hiki lilichogubikwa na kiwingu cha huzuni kufuatia kifo cha mwanasiasa huyo ambaye amewahi kutumikia UVCCM katika nyadhifa mbali mbali ikiwemo mwaka  1989  aliteuliwa kuwa Katibu Msaidizi Idara ya Fedha na uendeahaji Makao Makuu UVCCM, mwaka 1993 akawa Katibu msaidizi Mwanadamizi Idara ya Oganaizesheni na Utawala akishughulikia Utumishi UVCCM Makao Makuu.

Kutoka na juhudi ari na moyo wa kujituma Marehemu Feruzi Mwaka huo huo akapandishwa daraja na kuwa Mkuu wa kitengo cha Utumishi UVCCM Makao Makuu ambapo mwaka 1994 aliteuliwa kuwa Katibu Msaidizi UVCCM Afisi Kuu Zanzibar na Mwaka 1999 aliteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu wa UVCCM Zanzibar na baadae  aliteuliwa Naibu Katibu Mkuu CCM Zanzibar kazi ambayo alifanya kwa mafanikio makubwa akidhihirishia ulimwengu kuwa amepita na kuokwa katika tanuri la kuandaa viongozi  (UVCCM) kama ilivyokuwa kwa viongozi wengine katika chama na Serikali. 

Mungu ailaze mahali pema roho ya marehemu Saleh Ramadhan  Ferouz peponi.

Inna Lilahi wa Inna Ileihiy Rajiun

Chapisha Maoni

0 Maoni