Unordered List


MAKALA: ALAMA KUU ZA SERIKALI YA AWAMU YA TANO CHINI YA RAIS MAGUFULI “THE AFRICAN BULLDOZER”

Na Felician Andrew
Chuo Kikuu Mzumbe, Morogoro.
Ni takribani miaka minne sasa toka Rais Dkt. John Pombe Magufuli ameingia madarakani kama kiongozi wa juu kabisa katika taifa la Tanzania. Safari ya Rais Magufuli hata kufika kwenye nafasi hii ilijawa na vizuizi vingi njiani kiasi ambacho ilifanya asiwepo mtu yeyote ambaye angeweza kubashiri na kuamini kuwa leo hii ndiye angekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Lakini vizuizi hivi vilivyokuwepo ndio leo hii watu wengi wameanza kuviona na kuamini kama njia sahihi ya kupatikana kiongozi mzalendo, jasiri na mwenye mapenzi ya dhati na nchi yake.
Rais Magufuli alianza kuliongoza Taifa hili likiwa limepasuka vipande viwili vilivyotokana na mipasuko ya kisiasa lakini kwa ujasiri na ushapavu wake leo hii tunaongea kama taifa moja tukiimba wimbo mmoja tu wa Uzalendo na kusonga mbele kama taifa.
Baada ya kuyaona hayo hapa ni mfululizo wa mambo makubwa ambayo Rais Magufuli ameweza kuyafanya ndani ya muda wa miaka minne pekee ya uongozi wake na kuvuka matarajio ya watu wengi ndani na nje ya nchi.

1.            Kufufua Shirika la Ndege la Umma
Hali ya shirika la Ndege la Tazania ilikuwa mbaya na kutajwa kuwa limefilisika huku likishindwa kujiendesha kwa muda mrefu kutokana na kushindwa katika biashara na mwisho kujiendesha kwa hasara.
Tangu Rais Magufuli ameingia madarakani; Shirika la Ndege la Tanzania ATCL limefanikiwa kupunguza hasara iliyopatikana mwaka wa fedha 2015/16 ya shilingi billioni ishirini hadi kufikia shilingi billioni 4.4 katika mahesabu yake ya mwaka wa fedha 2016/17 ikiwa ni mwaka mmoja tu toka serikali ianze rasmi jitihada za kulifufua shirika hilo.
Aidha maboresho hayo yamechangia kukua kwa biashara ndani ya shirika hilo, ambapo hivi sasa ATCL inamiliki soko la ndani kwa zaidi ya asilimia 24 na sasa shirika limekuwa na nguvu na kuongeza utendaji pamoja na kuajiri watumishi wengi zaidi ili kuweza kujiendesha katika ulimwengu wa biashara za ushindani.


2.            Ununuzi wa ndege nane za kisasa
Mpaka kufikia mwaka 2015 shirika la ndege la Air Tanzania lilikuwa na ndege moja tu aina ya Bombardier DASH8 Q300 ambayo imekuwa ikihudumu kutokea mwaka 2011. Lakini katika kipindi cha miaka mitatu ya Rais Magufuli tumeshuhudia ununuzi wa ndege sita mpaka sasa ambayo inafanya shirika hili kuwa na jumla ya ndege saba hadi kufikia Disemba mwaka 2018.
Ndege zilizopo mpaka sasa zinajumuisha Bombardier DASH8 Q400 tatu, mbili ambazo zilifika Tanzania Septemba 2016 na moja Juni 2017; Bombardier CS300 mbili na Boeing 787 Dreamliner ambazo zilitua nchini kati ya mei na Julai 2018.
Aidha sasa serikali imejipanga kuingiza ndege nyingine ya nane ili kuweza kushindana na mataifa mengine katika eneo la Usafiri wa anga kwa mashirika yaliyochini ya serikali, ndege hii tayari serikali imekwishawasilisha bungeni maamuzi yake ili yaweze kubarikiwa na bunge katika bunge la Bajeti linaloandelea na Tanzania chini ya Rais Magufuli itasimama tena kwenye kilele cha mlima Kilimanjaro kupeperusha bendera ya mafanikio katika sekta hii ya Usafirishaji wa anga kwani shirika letu la ndege lilikuwa limekufa kabisa lakini sasa limeanza safari kwenda nchi za mbali na bara la Afrika.


3.            Elimu Bure
Baada ya muda mrefu tokea Uhuru Rais Magufuli amekuwa Rais wa kwanza wa Tanzania kuthubutu kufuta ada na michango yote kwa kuanzia shule ya Msingi hadi Sekondari. Maamuzi haya yameendana na utekelezaji wa malengo ya milenia ambayo yalijikita kwenye upatikanaji wa Elimu kwa watu wote.
 Kwa kufanya hivi serikali ya awamu ya tano imekuwa ikitumia bilioni 18 kila mwezi kwa ajili ya kugharamia elimu bure nchini ili kuweza kuhakikisha elimu haitolewi kwa ubaguzi nchini na watoto wote wa kitanzania wanafanikiwa kwenda shule na kusoma kama urithi sahihi na njia ya kuutokomeza umasikini.

4.            Mishahara hewa na wafanyakazi hewa
Kwa muda mrefu nchi yetu imekuwa ikipoteza fedha nyingi kwenye kulipa wafanyakazi hewa huku fedha hizi zikiwa zinaenda kwenye mifuko ya watu wachache wasiostahili kwa mfano mwaka 2013/2014 jumla ya shilingi Bilioni 1.62 zilitumika kulipa mishahara hewa kwa watumishi hewa huku katika mwaka 2015/2016 jumla ya shilingi bilioni 7.3 zilitumika kulipa mishahara hewa na kufanya serikali kuokoa Jumla ya shilingi bilioni 15 mpaka kufikia mwisho wa mwaka 2017.
Tangu ameingia madarakani Rais Magufuli amefanikiwa kufuta na kuondoa tatizo hili kwa kuwabaini wafanyakazi hewa wote na kusitisha mianya ya mishahara hewa iliyokuwa imekithiri nchini na kuokoa fedha hizi nyingi zilizokuwa zikipotea na kuibiwa.
 

5.            Kuondoa wafanyakazi wengi wenye Vyeti feki
Jambo jingine la kijasiri kufanywa na Rais Magufuli ni msimamo wake katika kuhakikisha watu wote waliokuwa wameajiliwa kwa vyeti feki kutolewa kwenye utumishi wa umma na kuokoa fedha nyingi ambazo serikali ilikuwa ikitumia kuwalipa wafanyakazi ambao wamekuwa wakichukua nafasi wasizostahili huku wale wanaostahili wakiwa wako nje ya mfumo wa ajira.
Mpaka kufikia April 2017 jumla ya wafanyakazi wenye vyeti feki 9,932 walikuwa wameondolewa ili kupisha nafasi hizo kuchukuliwa na watu wengine wenye sifa na waliostahili.
Uamuzi huu wa kijasiri unatajwa uwa moja kati ya matukio shupavu na yenye maamuzi magumu kuwahi kufanywa na viongozi wa juu wa serikali barani Afrika na duniani kote.
 

6.            Msimamo kwenda kwenye Uchumi wa Kati na Viwanda
Kwa muda mrefu mipango ya serikali ilikuwa ikiishia kwenye makaratasi lakini Rasi Magufuli amesimama kidetet kuona sasa kunakuwa na utekelezaji wenye tija wa mipango yote ya serikali.
Uwekezaji kwenye Viwanda ulikuwa kwa kasi wakati wa uongozi wa Baba wa Taifa lakini baadae Viwanda vingi vilikufa na mwisho ndoto ya muda mrefu yya taifa hili ikayeyuka lakini Rais Magufuli aliweka wazi msimamo wake wa kubadili muelekeo wa uchumi wa Tanzania na kuanza ujenzi wa taifa la Viwanda kwa nguvu kubwa huku wawekezaji wakipewa vipaumbele kuwekeza kwenye maeneo mbalimbali nchini.
Aidha serikali iliweka mipango mbalimbali kuhakikisha inafikia malengo ya Viwanda ikiwemo kil amkoa kuwa na Viwanda 100 na hii ilifanya mikoa kushindana kufikia malengo ya kitaifa ambapo kwa kipindi cha miaka miwili pekee ya utumishi wa Rais Magufuli jumla ya Viwanda 3,600  vikijumuisha Viwanda vikubwa, vya kati na vidogo vilikwishakuanza kazi ya uzalishaji huku zaidi ya viwanda 200 vikiwa vimeanzishwa huko mkoani Pwani.



7.            Kufuta safari za nje
Mara baada ya kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dr. Magufuli aliamua kufuta safari zote za nje kwa watummishi na viongozi wa serikali huku yeye mwenyewe akiwa mfano kwa kutosafiri kwenda nje ya nchi na kujikita katika utatuzi wa shida za wananchi huku akiamini ya kuwa amechaguliwa kuwatumikia watanzania hivyo jukumu lake la msingi ni kusimamia maslahi ya watanzania. Mbali na mialiko mbalimbali ambayo Rais Magufuli amepokea kutoka kwenye mataifa mbalimbali duniani lakini ameendela kusimamia msimamo wake na kuhakikisha analinda fedha za umma kwa kupunguza kabisa safari za nje zisizo na ulazima.
Rais Magufuli akihutubia bunge kwa mara ya kwanza na kufungua Bunge la 11 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mnamo tarehe 20 Novemba 2015 alisema ya kuwa “Katika mwaka 2013/14 na 2014/15 pekee serikali ilitumia Jumla ya shilingi Bilioni 356.324 kwa ajili ya safari za nje ya nchi” hata hivyo Rais Magufuli aliwaambia wabunge ya kuwa atahakikisha safari zinadhibitiwa ili fedha hizi zikatumike katika ujenzi wa miundombinu imara na kutumika katika uimarishaji wa huduma za kijamii ili kujenga uchumi imara. 
 

8.            Serikali Kuhamia Dodoma
Maamuzi ya Rais Magufuli kuhakikisha ndoto ya baba wa TAIFA Mwl. Julius Kambarage Nyerere inatimia limekuwa ni jambo kubwa sana ambalo watu wengi hawakuamini kama litafanikiwa lakini kwa umakini na ushapavu wa Rais Magufuli jambo hili limewezakana na mwezi Aprili 2019 imehitimisha kilele cha serikali na mashirika yake ya umma kuhamia katika mji wa Dodoma.
Aidha, uwepo wa Ofisi ya za serikali mjini Dar es Salaam ulikuwa ni mzigo mkubwa kwa serikali kwani serikali ilikuwa inatumia gharama nyingi kwa ajili ya kulipia kodi kwa ajili ya pango kwa Ofisi zake na taasisi zake nyingi.
Mfano, kwa mujibu wa ukaguzi wa CAG mnamo mwaka 2012/13 serikali ilikuwa ikitumia jumla ya shilingi za kitanzania Bilioni 7.9 kwa ajili ya kulipia kodi za pango kwa ofisi za serikali ndani ya mji wa Dar es salaam lakini leo hii ofisi za serikali zinahamia Dodoma kwenye mji wa serikali ambapo kodi hizi zote sasa zitakuwa zimekufa hivyo jambo hili limeweka historia kubwa katika matumizi sahihi na ulinzi wa fedha za umma kwa kupunguza matumizi ambayo yamo ndani ya uwezo wa serikali kuepukika.





 

9.            Ujenzi wa Reli ya Kisasa ya Standard Gauge
Mwaka 2017 unasimama kama mwaka wa kihistoria katika nchi ya Tanzania baada ya serikali chini ya Rais Magufuli kuamua kuanza ujenzi wa reli ya kisasa inayotumia umeme. Maamuzi ya ujenzi huu yanamfanya Rais Magufuli kuacha alama zitakazodumu na kukumbukwa miaka yote nchini kama muasisi wa mabadiliko makubwa ya miundombinu na Usafirishaji nchini. Aidha, ujenzi huu kutokana na umuhimu wake utaenda kwa kasi ya haraka huku ukiwa chini ya wakandarasi kutoka mataifa ya Uturuki pamoja na Ureno.
Mradi huu wa ujenzi wa reli ambao utagharamu jumla ya fedha za kitanzia shilingi trilioni 2.7 utakuwa na uwezo wa kubeba mizigo ya zaidi ya tani 30 itakuwa na uwezo wa kukimbia kwa mwendokasi wa km 160 kwa saa ambayo ujezi wake umeanzia katika mkoani  Dar es Salaam na kuishia Morogoro kwa awamu ya kwanza ikiwa ni Jumla ya kilometa 300, na kutoka Morogoro hadi Makutupora mkaoni Dodoma sawa na umbali wa kilometa 422 lakini malengo yakiwa kuhakikisha tunafika hadi nchini Rwanda ili kupanua wigo wa biashara ya usafirshaji hasa mizigo kwenda katika nchi zilizo mbali na bahari hindi.
Mradi huu mkubwa uatarajiwa kukamilika ifikapo Novemba 2019 kwa kipande cha Dar es Salaam mpaka Morogoro na kufika kukamilika kwa Mradi wote mpaka 2020 huku maeneo mengine yatakayonufaika na reli hii ya umeme ni pamoja na Makutupora –Tabora (km 295), Tabora –Isaka (km 133), Isaka –Mwanza (km 250), Tabora –Uvinza –Kigoma na Kaliua –Mpanda.
 

10.          Mageuzi makubwa katika miundombinu ya Usafirishaji nchini
Rais Magufuli anaandika historia nyingine muhimu katika nchi ya Tanzania kwa kuhakikisha zinajengwa barabara za juu na kusimamia matumzi ya fedha za umma kwa vitendo.
Hadi kufikia mwezi Machi 2019 tayari ujenzi ulifikia asilimia 25 hivyo ujenzi huu unatajwa kuwa moja kati ya miradi ambayo itamaliza kabisa tatizo la foleni na kurahisisha Usafiri ndani ya jiji la Dar es Salaam ambao utaendana na Upanuzi wa barabara na kufikia njia sita ambao unalenga kuongeza kasi na ukubwa wa biashara ya Usafirishaji nchini huku ujenzi huo tayari umeshaanza na malengo ni kujenga barabara hizo za njia sita kutoka Kimara mkoa wa Dar es Salaam hadi Chalinze mkoani Pwani na baadae kwenda hadi mkoani Mororgoro itakayokuwa na urefu wa kilometa 200.
Kukamilika kwa miradi hii mikubwa kutaacha alama nyingine kwani kunaleta mageuzi makubwa ya miundombinu katika nchi ya Tanzania na kuboresha biashara ya Usafirishaji ambayo ndio biashara inayokuwa kwa kasi zaidi duniani kote.
Kwa mujibu wa TANROADS barabara za kupishana juu yaani Ubungo Interchange zinatarajiwa kukamilika ifikapo Disemba 2020 huku miradi hii ikijengwa kwa kutumia fedha za watanzania.
Aidha; Mapinduzi haya ya ujenzi yalianza baada ya kukamilika kwa daraja la juu la Mfugale lililogharimu dola milioni 42 mpaka kukamilika kwake.
Mageuzi makubwa katika miundombinu kwa kipindi cha miaka mitatu ya Rais Magufuli kimepelekea mageuzi makubwa, mathalani katika kipindi cha Julai, 2017 hadi Machi, 2018, jumla ya tani 276,769 za mizigo zilisafirishwa ikilinganishwana tani 217,331 zilizosafirishwa katika kipindi kama hicho mwaka 2016/2017. Hili ni sawa na ongezeko la asilimia 27 hivyo kuna tija kubwa ya kuboresha miundombinu ya usafirshaji ili kupanua biashara hii nchini.
11.          Barabara za kisasa mikoani kuunganisha nchi nzima
Katika kipindi cha miaka mitatu serikaliya awamu ya tano chini ya Rais Magufuli imetengeneza barabara pamoja na madaraja mengi kuunganisha sehemu mbalimbali za nchi pamoja na huduma za jamii kwa wananchi huku madaraja na barabara hizizikiwa ni vichocheo vikubwa vya Maendeleo kwa kuhakikisha wananchi wanapata nafasi ya kushiriki kwenye shughuli za maendeleo.
Mathalani hadi kufikia mwezi machi 2018 jumla ya kilometa 17,055 za barabara zilikuwa zimekwishafanyiwa ukarabati huku jumla ya madaraja 996 nayo yalikuwa yanaendelea na ukarabati ili yaweze kupitika nyakati zote. Kwas iku za hivi karibuni Tanzania imeweka rekodi nyingine ya ujenzi wa barabara iliyo juu kuliko barabara zote Afrika kutokakwenye usawa wa bahari ambayo ina urefu wa kilometa 72 inayotoka Mbeya kuelekea Chunya sanjari na barabara hii tayari daraja la mto sibiti limekamilika kufuatia maagizo ya Rais Magufuli kupitia ziara zake baada ya ujenzi huo kusuasua kwa muda mrefu.

12.          Miradi mikubwa ya Maji kuondoa kero za maji nchini (Mradi wa Ziwa Victoria)
Mradi wa maji ya ziwa victoria unakuwa ni muarobaini wa shida za maji kwa wananchi wa kanda ya Kati hasa Tabora na miko ya jirani.
Mnamo mwaka 2017 serikali iliamua kuingia makubaliano na makampuni kutoka nchini india kama sehemu ya wakandarasi watakao tekeza mradi huo mkubwa wa maji uliotumia zaidi ya shilingi za kitanzania bilioni 600 huku mji wa Nzega ukipewa heshima ya kuwa kituo kikuu cha usambazaji wa maji ya ziwa Victoria.
Mradi wa maji wa ziwa Victoria uatarajiwa kutoa maji kwenye mikoa ya Shinyanga, Tabora na kuelekea hadi Singida. Aidha Rais Magufuli pia akiwa mkoani Simiyu aliweza kutoa fedha Jumla ya shilingi bilioni 340.2 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa mradi wa maji kwenye mkoa huo kwa kutimia maji kutoka Ziwa Victoria.
Aidha, pia serikali imeweza kusaini mkataba mwingine wa mradi mkubwa wa Maji wa Nyashimo wilayani Busega wenye thamani ya shilingi bilioni 1.8.
Jitihada zote hizi zinefanywa na serikali ili kuhakikishainaondoa kero kuu za maji kwenye maeneo mbalimbali nchini na kuhakikisha maji yanapatikana kwa urahisi zaidi.
               
13. Utekelezaji wa Mradi ya Umeme wa Kinyerezi I, II, III na IV
Mnamo 3 Aprili 2018, Rais Magufuli alizindua Mradi wa Kinyerezi II uligharmu jumla ya fedha za kitanzania shilingi bilioni 700. Mradi huu ulianza utekelezaji wake kuanzia 1 Machi 2016 na miaka miwili baadae  kukamilika ambapo serikali iliwekeza katika matumizi ya teknolojia ya kisasa ya uzalishaji wa umeme kwa kutumia gesi asilia kutokea mkoani Mtwara ijulikanayo kama Combine Cycle.

Mradi huuwa Kinyerezi II una uwezo wa kuzalisha hadi megawatt 240 ambazo zitaingizwa kwenye grid ya taifa.
Aidha, Rais aliwezesha utekelezaji wa mradi wa umeme wa Kinyerezi I mwaka 2016 ambao unaendelea kupanuiwa ili uweze kuzalisha megawatt 185 na unatarajiwa kuzinduliwa mwaka huu 2019 mwakani na utagharimu kiasi cha dola milioni 180 zote zikiwa ni fedha za ndani.
Lakini pia kutakuwa na Kinyerezi III kituo ambacho kitazalisha megawtt 600 za umeme na mradi huu utatekelezwa kwa awamu mbili huku Kinyerezi IV inatarajiwa kuzalisha megawatt 450. Aidha ndani ya muda mfupi wa miaka miwili yaani 2016 hadi 2018 tayari serikali ilifanikisha kuwaunganisha wananchi umeme kutoka milioni 1,054,000 hadi 2,014,000 ikiwa ni ongezeko la asilimia 30 na matokeo makubwa yanaendela kuonekana kupitia utekelezaji wa mradi wa umeme vijiji REA III.
 

14.          Mradi mkubwa wa umeme maarufu kama Stigler’s Gorge (Wa 2 kwa ukubwa Afrika)
Rais Magufuli kwa mara nyingine anaingia katika historia ya Tanzania kwa kuidhinisha utekelezaji wa mradi wa uzalishaji wa umeme katika neo la mto Rufiji ujulikanao kama Stigler’s Gorge. Mradi huu ni matokeo ya utafiti uliofanywa kwa zaidi ya miaka 40 iliyopita.
Mnamo Disemba 2018, Rais Magufuli ilisaini kandarasi ya ujenzi wa Mradi huu mkubwa wa uzalishaji umeme na serikali ya Misri kupitia Waziri Mkuu wa nchi hiyo pamoja na makampuni yaliyofanikiwa kupata nafasi ya ujenzi wa Mradi huu mkubwa wa uzalishaji umeme.
Mradi huu unatarajiwa kutekelezwa na fedha za watanzania wenyewe kwa kiwango cha dola za kimarekani bilioni 2.9 ambayo ni sawa na takribani shilingi trilion 6.5 za kitanzania huku ukitarajiwa kuwa na uzalishaji wa megawatt 2100.
Kukamilika kwa mradi huu kutaifanya nchi ya Tanzania kuwa nchi ya 2 yenye mradi mkubwa zaidi  wa uzalishaji wa umeme barani Afrika ikiwa nyuma ya Ethipoia.
Ushapavu wa Rais Magufuli ulionekana baada ya kuweza kuwashinda mataifa mbalimbali ya ulaya ambayo yalikuwa yakipinga utekelezaji wa Mradi huu huku yakijua fika ya kuwa Tanzania ina uhaba wa nishati ya umeme na pia tunahitaji umeme ili kufanikisha maelengo na dira ya Taifa ya kuwa taifa la viwanda na uchumi wa kati.
Hata hivyo wataalamu mbalimbali wanasoma bonde hili lilipo kwenye mto Rufiji linafanana kwa ukaribu na lile la Canyon lililopo nchini Marekani.
Utafiti uliofanywa miaka ya sabini na mwanzoni mwa miaka ya themanini (1978-1980) na Shirika la Kuendeleza Bonde la Mto Rufiji (RUBADA ) kwa kushirikiana na kampuni ya kigeni ya M/s Norplan/Hafslund, ulionyesha kuwa mradi wa Stiegler’s Gorge una uwezo mkubwa wa kuzalisha umeme mwingi wa maji (hydro-power) zaidi ya umeme ambao Tanzania inahitaji.
Hivyo, Stiegler’s Gorge, ambayo kwa taarifa za satellite inapatikana umbali wa kilomita 185 kutokea jijini Dar es Salaam, kwa sasa inaangaliwa kama kitovu kitarajiwa cha kuimarisha mzizi mkuu wa  uchumi kuelekea Tanzania mpya tuitakayo kwani mradi huo ukikamilika, ikichanganywa na megawati 1,460 zinazozalishwa sasa na megawati 600 zinazozalishwa kutoka miradi ya Kinyerezi I, II, III na IV nchi itaweza kuzalisha megawati zaidi ya 4,000 hadi 5,000.
 

15.          Ongezeko kubwa la Mapato na Ukuaji wa uchumi kwa asilimia 7
Rais Magufuli amekuwa ameendelea kuandika historia ya aina yake nchini Tanzania kufuatia usimamizi wake kwenye eneo la ukusanyaji wa kodi na kuondoa mianya mingi ya ukwepaji kodi ambao umekuwa ukifanywa na wafanyabiashara wasio waaminifu kwa muda mrefu.
Mpaka kufikia Juni 30 mwaka 2016 makusanyo yatokanayo na kodi yalipita malengo kwa asilimia moja huku fedha iliyokusanywa ilikuwa ni shilingi trilioni 12.363. Uvukaji wa malengo ulichangiwa na ongezeko la usimamizi mzuri na ufatiliaji wa Malipo ya kodi yaliyotokana na uboreshaji wa Mamlaka ya Mapato Tanzania.
Ukusanyaji wa kodi umeendelea kuimarika na kuwa msingi wa utekelezaji wa miradi mikubwa ya Maendeleo nchini. Nchi zote zilizoendela duniani ziliweza kuhakikisha zinaongeza Idadi ya waliapakodi na kupanua wigo wa kodi na vitu au mali za kulipiwa kodi lakini pia sababu za nchi nyingi kushindwa kuendelea kiuchumi ni pamoja na kuwa na mifumo mibovu ya ukusanyaji kodi.
Hivyo, kwa shauku ya Rais Magufuli kuona ya kuwa Tanzania inaendelea na kufikia viwango vikubwa vya ukuaji wa kiuchumi na Maendeleo ya watu ameamua kuhakikisha kila anayestahili kulipa kodi analipa kodi kwa maslahi ya taifa.
Aidha serikali ya Tanzania imeendelea tena kuwa miongoni wa serikali zilizotilia mkazo suala la Maendeleo ya kiuchumi kwa ajili ya ustawi wa taifa lake baada ya kuhakikisha nchi inaendelea kuwa na ukuaji wa uchumi unaopanda kwa muda wa miaka mitatu mfululizo ambapo ukuaji umekuwa kutoka asilimia 6.5% mwaka 2016  kwenda 6.8% mwisho wa mwaka 2017 na sasa kufikia kiwango cha 7% huku Rais wa IMF akiendelea kupongeza kazi kubwa inafanyw ana serikali ya Tanzania hasa  kupitia uwekezaji mkubwa kwenye sekta za nishati, maji, miundombinu na mbadiliko makubwa ya mifumo na udhibiti wa rushwa nchini.
 

16.          Uimarishaji Elimu ya Juu nchini
Mbali na serikali kuendelea kutoa Mikopo kwa wanafunzi, Rais Magufuli maeendela kuongeza uwekezaji wake katika sekta ya elimu ya juu nchini kwani ndio kisima cha wataalamu ambao ndio watashiriki katika ujenzi wa taifa la Viwanda.

Katika kipindi cha miaka mitatu miradi kadhaa kwenye vyuo vikuu imetekelezwa na serikali ya awamu ya tano ikiwemo ujenzi wa hosteli kwenye vyuo vikuu mbalimbali vya umma nchini kama sehemu ya kuboresha mazingira ya elimu nchini.
Aidha, kwa kipindi cha miaka mitatu tumeshuhudia ujenzi wa hosteli mpya katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Chuo Kikuu cha Mzumbe Morogoro na Mbeya pamoja na ujenzi wa Upanuzi wa chuo kikuu cha Sayansi na Teknolojia cha Mbeya.
Aidha serikali pia imeendela kugharamia vifaa vya kujifunzi na ujenzi wa Maabara za kisasa kwenye vyuo mbalimbali vya afya na tiba pamoja na vile vya Kilimo.
 
17.          Ujenzi wa daraja la kuvuka Bahari ya Hindi upande wa Salenda
Jambo jingine ambalo limeendelea kuishi kwenye kitabu cha matendo ya Tanzania wakati wa utumishi wa Rais Magufuli ni ujenzi wa daraja linalovuka bahari kwenye eneo la Salenda. Ujenzi wa daraja hili la kisasa unalenga kuondoa folein katikati ya mji na kuboresha mifumo ya Usafiri nchini ili kuhakikisha Dar es Salaam unabaki kama mji mkubwa wa kibiashara na kuongeza miundombinu ambayo itafanya kuongeza kwa utalii wa mijiji.
Aidha, utiaji saini wa zoezi hili ulifanyika tarehe 23 Julai 2018 na sasa ujenzi unaendelea na kuvutia sehemu ya watu wengi wanaopita njia hiyo kuona namna ujenzi wa daraja linalovuka bahari unavyokuwa na mpaka kukamilika kwa daraja hili lenye urefu wa kilometa 1.03 litakuwa na uwezo wa kupitisha magari elfu 50 kwa siku huku muda wa ujenzi mpaka kukamilika ukiwa ni miezi 36 pekee.


18.          Ujenzi wa daraja kuvuka ziwa Victoria
Kufuati uboreshaji wa miundombinu nchini Rais Magufuli alitanga kuanza ujenzi wa daraja kuvuka Ziwa Victoria ambalo linafahamika kama Daraja la Kigogo – Busisi.
Daraja hili litakuwa na urefu wa mita 3,200 sawa na kilometa 3.2, pamoja ujenzi wa barabara ya lami yenye urefu wa kilometa 1.66. Kufuati maamuzi hayo ya Rais tayari zabuni ilishatangazwa na ujenzi unategemea kukamilika ndani ya miaka 4.
Kukamilika kwa ujenzi wa daraja hili kutakuwa muarobaini wa Usafiri kwenye eneo hili ambako tumekuwa tukishuhudia vivuko vimekuwa vikipata shida na kusababisha madhara makubwa kwa wananchi.


19.          Ujenzi wa ukuta wa Merereni kulinda na kuzuia utoroshwaji wa madini nchini
Madini ya Tanzanite yanayoaptikana Tanzania pekee duniani kote lakini kw amiaka mingi masoko ya madini haya yamekuwa nje ya nchi hasa Kenya na India huku sehemu kubwa ya mapato yake yakiwa hayanufaishi nchi ya Tanzania.
Msimamo wa Rais Magufuli kuzungusha ukuta kuzunguka eneo la uchimabji ulilenga kuhakikisha kunakua na usimamiaji wa kutosha katika madini haya ya kipekee na yenye thamani kubwa nchini. Madini haya yalivumbuliwa na Bw. Jumanne Ngoma mwaka 1967 lakini tokea ugunduzi wake mpaka leo Tanzania haijanufaika sana kama mataifa mengine huku thamani ya mauzo ya madini haya duniani kwa mwaka ni dola za kimarekeni milioni 50.
Rais Magufuli aliamua kujenga Ukuta wenye urefu wa kilomita 24.5, mita 3 kwenda juu na mpaka kukamilika kwake umegharimu karibu ya shilingi bilioni 6 na kujengwa na maafisa wa jeshi pamoja na wanajeshi wengine 271 ambao baada ya kukamilika kwake Rais aliamua wanajeshi wote kuweza kupatiwa ajira za kudumu jeshini.

20.          Uanzishwaji wa masoko ya madini nchini
Kufuatia nchi ya Tanzania kutokunufaika na madini mengi yaliyopo nchini, Rais Magufuli aliamua kila mkoa unaozalisja madini kuanza mchakato wa ujenzi wa Masoko ya Madini ili kuhakikisha kama taifa linaweza kunufaika namadini hayo nakuzuia kabisa mianya yote ya utoroshaji wa madini nchini ambao umekuwa ukifanywa kwa muda mrefu na wafanyabiashara wasio waaminifu.
Mkoa wa Geita ulifanikiwa kufungua soko kubwa na baadae mikoa mingine imeendelea kujenga na kufungua masoko haya ambayo tunategemea yatajengwa kwenye vituo vyote muhimu vya biashara nchini ikiwemo bandarini na kwenye airport zote nchini.
Uanzishwaji huu wa masoko ya madini unaendana na utungwaji wa sheria kuhakikisha mambo yote muhimu yanarasimishwa ili kuweza kuwa na utaratibu sahihi wa kuhakikisha nchi inanufaika na rasilimali hizi muhimu.
Mpaka sasa tayari mikoa iliypofungua masoko ya madini nchini ni pamoja na Mwanza, Shinyanga, Mbeya, Morogoro, Kilimanjaro, Tabora na Arusha.

21.          Kupungua kwa rushwa iliyokuwa imekithiri nchini na watuhumiwa kufikishwa mahakamani na wengine kufungwa
Kwa mujibu wa mtandao wa Afrobarometer, rushwa imepungua sana nchini Tanzania katika awamu ya tano na hii inatokana na umahiri, ushupavu na msimamo wa Rais Magufuli katika kuichukia rushwa kwa vitendo kuliko pelekea kuimarisha Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa(TAKUKURU).
Ripoti ya Afrobarometer iliyotolewa Januari 2019 inaonyesha ya kuwa nchini Tanzania wananchi wengi wameongeza kiwango cha kuridhika na huduma zinazotolewa na serikali kwa zaidi aya asilimia 89 huku wakipongeza kupungua kwa urasimu katika upatikanaji wa huduma zitolewazo na mashirika ya umma

22.          Ujenzi wa Zahanati zaidi ya 352 na Hospitali za Wilaya 67 nchi nzima
Aidha katika kipindi cha miaka mitatu, Taifa limeshuhudia mageuzi makubwa katika sekta ya afya nchini ambapo tumeshuhudia Rais Magufuli akihakikisha vimejengwa vituo vya Afya 352 na ongezekola hospitali kubwa za wilaya 67 nchi nzima.
Ongezeko hili kwa kipindi cha miaka mitatu pekee ni kubwa sana na linafanya serikali ya awamu ya tano kuweka historia katika ameneo muhimu yanayogusa afya na maisha ya watanzania.
Kwa upande mwingine ili kuongeza msisitizo kwenye sekta ya afya Rais Magufuli ameidhinisha ongezeko la bajeti ya madawa kwenye sekta ya afya kutoka shilingi bilioni 31 hadi kufikia shilingi bilioni 270.
Hii ni sehemu ndogo ya matukio muhimu ambayo yamefanywa na serikali ya awamu ya tano kwa kipindi kifupi cha miaka mitatu ya utumishi wake na kuacha alama kubwa.
 

MWISHO
Baada ya Rais Magufuli, kukataa mkataba mbovu wa kinyonyaji uliokuwa unataka kuliingiza taifa la Tanzania kwenye jaribio la kuuza ardhi, mali na urithi wake kwa kampuni yeye historia ya kufilisi nchi mbalimbali barani Afrika na nchi nyingine zinaozendelea duniani sasa kila mtu ametega sikio kusikia ni jambo gani kubwa litafanywa na Rais Magufuli katika mwaka huu wa nne wa uongozi wake.

Chagua kuwa Mzalendo, Simama na Rais Magufuli

Chapisha Maoni

0 Maoni